Hapana: NHIF haijasitisha huduma kwa wagonjwa wenye shida ya upumuaji
- Imezushiwa mtandaoni kuwa imeondoa huduma ya malipo ya oksijeni na dawa kwa watu wenye changamoto ya upumuaji.
- Yasema hakuna mabadiliko yoyote kwa wananachama wake kuhusu huduma inazogharamia.
- Inafuatilia ili kubaini kama kuna ukiukwaji wa kimkataba wa utoaji huduma kwa wanachama wake.
Dar es Salaam. Mfuko wa Bima ya Taifa ya Afya (NHIF) umesema kwa sasa haujandoa huduma ya malipo ya oksijeni na dawa kwa watu wenye changamoto ya upumuaji kama inavyodaiwa na baadhi ya watumiaji wa mitandao ya kijamii.
Kauli ya NHIF inakuja baada ya kusambaa kwa taarifa katika mitandao ya kijamii ikiwemo Instagram zinazodai kuwa mfuko huo umeshitisha kugharamia huduma ya kupata hewa ya oksijeni na dawa kwa wanachama wake wanaokabiliwa na tatizo la upumuaji (pnemonia) na Corona.
Moja ya habari hiyo ambayo iko kwenye mtandao wa Instagram ikiwa na logo ya NHIF inaeleza kuwa, “Mfuko wa Bima ya Afya yaani NHIF yaondoa oxygen na dawa kwa wagonjwa wenye shida ya upumuaji na CORONA Ambapo inafikia laki 5 kwa dose”.
Hata hivyo, taarifa hiyo haina ukweli wowote na inalenga kupotosha kwa sababu NHIF tayari imetoa tamko na kubainisha hakuna mabadiliko yoyote ya huduma zake kwa wagonjwa wanaohudumiwa na mfuko huo.
“Mfuko kwa sasa haujaondoa huduma yoyote katika kitita cha mafao zikiwemo dawa aina ya Azithromycin, Vitamin C, Colchicine, Zinc Sulphate, Ciftriozone + Salbactam na heparin zinazolipiwa kama awali,” imeeleza taarifa ya mfuko huo iliyotolewa mapema leo Februari 15, 2020.
Zinazohusiana:
Hata hivyo, NHIF imeeleza kuwa inaendelea kufuatilia ili kubaini kama kuna ukiukwaji wa kimkataba wa utoaji huduma kwa wanachama wake wanaotibiwa katika hospitali mbalimbali Tanzania.
“Hivyo, taarifa zote zisizo rasmi zinazosambazwa zipuuzwe,” imeeleza taarifa ya NHIF iliyosainiwa na Kaimu Meneja Mahusiano wa mfuko huo, Catherine Kameka.
— NHIF Tanzania (@nhiftz) February 15, 2021
Latest