Hapana: Serikali haitakata pensheni za wastaafu kugharamia mfuko wa bima ya afya
- Waziri Ummy asema huo ni uzushi.
Dar es Salaam. Waziri wa Afya Ummy Mwalimu amesema taarifa zinazosambaa mtandaoni kuhusu Serikali kukata pensheni za wastaafu kugharamia Mfuko wa Taifa wa Bima ya Afya (NHIF), siyo za kweli.
Kumekuwa na taarifa ya uzushi inayosambaa mitandaoni inayodai kuwa Serikali itakata asilimia tano ya fedha za mafao ya uzeeni na kuzipeleka kwenye mfuko wa bima ya afya.
Uzushi huo unaosambazwa kupitia ukurasa wa Twitter wa Tanzania Abroad Tv unadai kuwa Serikali imefikia uamuzi huo ili kufidia uhaba wa fedha uliopo kwenye mfuko huo.

Soma zaidi:
Waziri Ummy kupitia ukurasa wake wa Instagram amesema taarifa hiyo haina ukweli wowote ni uzushi.
Huu ni uzushi. Ipuuzwe! Kufidia pesa??? Idara ipi ya Afya??? Fake News. https://t.co/fhLeJP7c2h
— Ummy Mwalimu,MP (@ummymwalimu) October 11, 2022
Katika siku za hivi karibuni kumekuwa na mjadala mpana kuhusu utendaji wa NHIF baada ya kuelemewa na madeni huku Serikali ikisisitiza mfuko huo utaendelea kutoa huduma.
Tayari, Serikali imewasilisha Bungeni muswada wa Bima ya Afya kwa Wote ambapo sheria yake ikipita utawawezesha Watanzania wengi kupata huduma za afya kwa uhakika.
Latest
Similar News