Sh2.1 bilioni kuwainua wakulima waliothirika na Corona Tanzania
- Zimetolewa na Mfuko wa Umoja wa Mataifa wa Maendeleo ya Kilimo (IFAD).
- Zitawasaidia wakulima wadogo zaidi ya 6,000 ambao wameathirika na janga la ugonjwa wa Corona na nzige wavamizi.
- Wakulima hao ni kutoka mikoa ya Dodoma, Njombe, Singida, Simiyu na Unguja.
Dar es Salaam. Huenda wakulima walioathirika na janga la Corona nchini Tanzania wakapata ahueni baada ya wadau wa maendeleo kutoa fedha zitakazowasaidia kupata mbegu bora na kuwekeza tena kwenye kilimo ili kujipatia kipato kuendeleza maisha yao.
Zaidi ya Dola za Marekani 882,841 (zaidi ya Sh1.1 bilioni) zimetolewa na Mfuko wa Umoja wa Mataifa wa Maendeleo ya Kilimo (IFAD) kwa ajili ya kusaidia wakulima wadogo zaidi ya 6,000 nchini Tanzania ambao wameathirika na janga la ugonjwa wa Corona pamoja na nzige wavamizi.
Wakulima hao ni kutoka mikoa ya Dodoma, Njombe, Singida, Simiyu na Unguja.
Ukuaji katika sekta ya kilimo nchini Tanzania ulikadiriwa kupungua kutoka asilimia 5 mwaka 2019 hadi asilimia 2 mwaka jana kutokana na COVID-19 pamoja na nzige wavamizi walioingia nchini humo na kuharibu mazao ya wakulima.
Majanga hayo mawili yameleta madhara ikiwemo kupanda kwa bei ya pembejeo za kilimo pamoja na wakulima wadogo kutofikiwa na masoko.
Athari hizo zinatishia kusukuma zaidi ya wakulima wadogo 500,000 kwenye lindi la umasikini.
Kuwainua wakulima hao, IFAD kupitia mfuko wake wa ruzuku ya kusaidia kupunguza umasikini (RPSF) umetoa Dola za Marekani 882,841 kusaidia Tanzania kuhimili madhara ya COVID-19 kwa wakulima.
“Janga la COVID-19 tumetudhihirishia mazingira magumu yaliyopo kwenye mifumo yetu ya chakula. Katika kuhakikisha tunajenga mifumo imara na endelevu ya chakula, tunatakiwa kutambua jukumu walilonalo wakulima wadogo na kuwawezesha kupata pembejeo za kilimo, taarifa za kilimo na masoko ya mazao yao” amesema Francesco Rispoli, Mkurugenzi wa IFAD nchini Tanzania.
Ili kusaidia kukuza uzalishaji wao, ruzuku hii inalenga kusambaza zaidi ya kilo 23,000 za mbegu za mahindi, zaidi ya kilo 14,000 za mbegu za alizeti pamoja na miche 971,000 ya matunda.
Wakulima watapatiwa mbolea, taarifa zinazohusiana na kilimo pamoja na masoko kupitia jukwaa la M-KILIMO linalowapatia wakulima taarifa kwenye simu zao za viganjani.
Makundi yatakayonufaika ni wanawake, asilimia 30 ni vijana na wengine ni wafanyabiashara wa mazao ya kilimo, wanunuzi, na maafisa ugani.
Licha ya changamoto nyingi wanazokutana nazo wakulima, sekta hii imebaki kuwa uti wa mgongo wa Taifa hilo na shughuli kuu ya kiuchumi kwa wakulima wengi wadogo nchini Tanzania.
Tangu mwaka 1978, IFAD imesaidia programu16 nchini Tanzania zenye thamani ya Dola za Marekani milioni 917 (Sh2.2 trilioni) ambazo zimewanufaisha moja kwa moja zaidi ya kaya milioni 4.
Latest