Ufaulu kidato cha sita 2021 wapanda kwa asilimia 0.11
- Umepanda kutoka asilimia 97.74 mwaka 2020 hadi asilimia 97.93 mwaka huu.
- Asilimia 99.05 ya watahiniwa waliofanya mtihani huo wamefaulu.
- Watahiniwa 78,251 sawa na asilimia 97.93 wamefaulu katika daraja la I hadi III.
Dar es Salaam. Katibu Mtendaji wa Baraza la Taifa la Mitihani (NECTA) Dkt. Charles Msonde amesema ufaulu katika matokeo ya mtihani wa kidato cha sita kwa mwaka 2021 umepanda kwa asilimia 0.11 huku shule za Serikali zikichuana vikali na za binafsi.
Akitangaza matokeo hayo visiwani Zanzibar leo Julai 10, 2021, Dkt Msonde amesema ufaulu wa jumla umepanda kidogo kwa asilimia 0.11 ambapo mwaka 2020 ulikuwa 99.51 na mwaka huu ufaulu ni asilimia 99.62.
Ufaulu huo ni sawa na ongezeko la asilimia 0.11.
Watahiniwa 89,802 walisajiliwa kufanya mtihani wa kitado cha sita Mei mwaka huu wakiwemo wasichana 38,018.
“Kati ya watahiniwa waliosajiliwa, watahiniwa wa shule walikuwa 81,143 na watahiniwa wa kujitegemea walikuwa 8,659,” amesema Dk Msonde.
Watahiniwa 87,043 sawa na asilimia 99.05 ya watahiniwa waliofanya mtihani huo wamefaulu, kati yao wasichana ni 37,322.
Ufaulu umepanda kidogo kutoka asilimia 98.35 ya watahiniwa 88,440 waliofaulu mtihani huo mwaka 2020.
“Ubora wa ufaulu kwa kuangalia madaraja waliyopata watahiniwa wa shule unaonesha kuwa jumla ya watahiniwa 78,251 sawa na asilimia 97.93 wamefaulu katika daraja la I hadi III wakiwemo wasichana 34,065 sawa na silimia 97.99 na wavulana 44,186 sawa na asilimia 97.89,” amesema Dk Msonde wakati akitangaza matokeo hayo.
Matokeo hayo yanaonyesha waliopata daraja la mwisho au ziri ni wanafunzi 306 sawa na asilimia 0.38.
Ufaulu wa mtihani wa kidato cha sita ni daraja kwa wanafunzi wanaoendelea na masomo ya elimu ya juu ili kwenda kusomea taaluma zao.
Latest