Serikali kukusanya zaidi ya Sh250 bilioni maduhuli ya ardhi kidijitali
- Fedha hizo zitatokana na kupima viwanja na kutoa hati.
- Hati miliki 2.4 milioni za ardhi kutolewa kwa wananchi.
Mwanza. Wizara ya Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi inatarajia kukusanya zaidi ya Sh250.1 bilioni kutokana na maduhuli ya sekta ya ardhi kwa kutekeleza mikakati mbalimbali ikiwemo kupima viwanja na kutoa hati miliki.
Njia itakayotumika kukusanya fedha hizo ni kwa kutumia mifumo ya kidijitali.
Miongoni mwa vipaumbele vitakavyosaidia kukusanya maduhuli hayo ni pamoja na kutoa hati miliki 2.4 milioni kwa wananchi ambao watapimiwa maeneo yao na kwamba hadi mpaka sasa hati hizo zimeshaandaliwa.
Mabula ametoa ufafanuzi huo Julai 12, 2022 kwenye mkutano wa waandishi wa habari jijini Mwanza uliolenga kutoa ufafanuzi juu ya utekelezaji wa vipaumbele vya bajeti ya Wizara ya Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi kwa mwaka 2022/23.
Soma zaidi:
-
Serikali ya Tanzania kupitia upya mfumo wa kodi
-
Waziri atangaza msamaha wa kodi ya ardhi kwa taasisi za dini
Dk Mabula amesema hadi sasa zaidi ya hati 24,000 nchi nzima za watu ambao wamekamilisha kulipia zimeshakamilika kwenye ofisi za wasajili lakini hawajaenda kuzichukua huku akieleza wasiwasi wake kuwa ni kutokana na uelewa wa kutosha wa watu kupata hati hizo.
“Changamoto iliyopo ni baadhi ya wananchi kushindwa kulipia hati hizo baada ya kupimiwa, takwimu zinaonyesha kuwa zaidi ya watu 900,000 nchi nzima wameshapimiwa lakini hawajalipia kupata hati zao,” amesema Mabula.
Amesema kutokana na changamoto hiyo mwaka jana walipitisha sheria kila mwenye kiwanja kipimwe na kuanza kulipiwa kodi na hii haijalishi kama kina hati au hakina jambo ambalo linatekelezeka.
Aidha, Mabula amewataka wananchi kushiriki kikamilifu kwenye suala la urasimishaji wa makazi ili kupunguza migogoro ya ardhi.
Amesema zoezi hilo lililoanza mwaka 2015 linatarajiwa kukamilika mwaka 2023 na kwamba kumekuwepo na changamoto ya baadhi ya wananchi kutoshiriki katika zoezi hilo ili maeneo yao yaweze kutambuliwa.
Latest
