Polisi: Tumewadhibiti ‘Panya road’ kwa asilimia 87 Dar
- Kamanda Murilo asema Dar ipo salama.
- Jeshi hilo bado linaendelea na msako wa wahalifu jijini hapa.
- Wanajamii, wananchi watakiwa kutafuta suluhu ya kudumu.
Dar es Salaam. Kamanda wa Polisi Kanda Maalum ya Dar es Salaam Jumanne Murilo amesema Jeshi la Polisi limefanikiwa kudhibiti vikundi vya wahalifu maarufu kama “panya rodi” kwa asilimia 87 huku akieleza kuwa kwa sasa hali ni shwari kwenye jiji hilo.
Kamanda Murilo alikuwa akizungumza kwenye mjadala wa kitaifa juu ya hali ya usalama na jitihada za Jeshi la Polisi katika kuwadhibiti ‘panya road’ katika Mikoa ya Dar es Salaam, Mwanza, Mbeya, Arusha na Dodoma ulioandaliwa na Watch Tanzania ambao umefanyika leo Octoba 3, 2022 kupitia mtandao wa zoom.
Amesema jeshi hilo linaendelea kufanya msako ili kudhibiti vitendo vya kihalifu jijini hapa.
“Asilimia 87 tumefanikiwa hii 13 bado tunaendelea nayo mpaka wananchi wasahau hili suala linaitwa panya road au masuala mengine ya kihalifu warudi kwenye shughuli zao nyingine za kiuchumi, kisiasa na kijamii,” amesema Kamanda Murilo.
Murilo amesema asilimia 13 za udhibiti zilizobakia wameshindwa kuzikamilisha kutokana na wahalifu hao kukimbia na kuhama kutoka kwenye maeneo yao ambayo jeshi hilo lilikuwa linayafahamu.
Septemba 18, 2022 Jeshi la polisi lilitoa taarifa ya kuuwawa kwa watu sita waliodaiwa kuwa ni panya road kwa kujihusisha na vitendo vya uhalifu wa kutumia silaha eneo la Makongo.
Akizungumizia jambo hilo, Kamanda Murilo amesema operesheni wananazoziendesha kusaka makundi ya kihalifu zinazingatia haki za binadamu na Jeshi la Polisi halina nia ya kuwaua wahalifu bali kuzuia vitendo viovu wanavyovifanya.
Soma zaidi
-
Samia ‘alipa makavu’ Jeshi la Polisi, alitaka kufanya mageuzi makubwa
-
Ashikiliwa na polisi kwa kumtorosha mtoto kunusuru ndoa yake
Wanafamilia, wanajamii tutafute suluhisho
Kamanda Murilo amesema ili kudhibiti wahalifu kama panya road ni vyema wanafamilia na jamii kwa ujumla wachukue hatua ili kupata suluhisho la kudumu la kutatua changamoto hii kwa sababu wahalifu wanatokea kwenye familia na kwenye jamii tunazoishi.
“Tatizo linaanzia kwetu wanafamilia na wanajamii kwa sababu sisi ndiyo tuna fursa nzuri ya kuona wanafanyaje mpaka wanajiingiza kwenye vitendo vya kihalifu,” amesema Muliro.
Amesisitiza kuwa jitihada za pamoja zinahitajika kuwadhibiti wahalifu wakiwemo panya road licha ya kuwa kazi yao ni kuwakamata na kuwafikisha katika vyombo vya sheria.
Latest