Wizara tano zenye bajeti ndogo mwaka 2023-24

June 8, 2023 12:47 pm · David
Share
Tweet
Copy Link
  • Wizara ya Utamaduni, Sanaa na Michezo pamoja na Wizara ya Madini ni miongoni.
  • Jumla ya fedha za bajeti kwa wizara tano ni sawa na nusu ya bajeti ya Wizara ya Maliasili na Utalii.
  • Kamati za Bunge zasema haziridhishwi na bajeti hizo.

Dar es Salaam, Macho na masikio ya Watanzania yapo bungeni jijini Dodoma ambako Serikali inatarajia kuwasilisha  bajeti yake  Juni 15, 2023 ambapo tayari wizara zote zimeshaidhinishiwa maombi ya fedha walizoomba kwa ajili ya shughuli za maendeleo na matumizi ya kawaida.

Wakati Serikali ikiwa mbioni kufanya majumuisho ya Bajeti kuu ya Serikali itakayosomwa wiki kesho bungeni jijini Dodoma, baadhi ya wizara zimeambulia fedha kiduchu kulinganisha na wizara nyingine.

Licha ya kutofautiana kwa ukubwa pamoja na wingi wa majukumu ni wazi kuwa kila wizara ina umuhimu wake kwa Taifa, hivyo fedha hizo kiduchu zinaweza zisitosheleze katika utekelezaji wa shughuli za maendeleo jambo litakalokwamisha ukuaji wa uchumi kwa taifa na mtu mmoja mmoja.

Zifuatazo ni wizara ambazo mara nyingi zimekuwa zikipata fedha ndogo kwa ajili ya kutekeleza majukumu yao ya kawaida na miradi ya maendeleo.

Waziri wa Utamaduni Sanaa na Michezo Pindi Chana alipokuwa akisoma bajeti ya wizara hiyo bungeni jijini Dodoma,PichalWizara ya Utamaduni

1.Wizara ya Utamaduni, Sanaa na Michezo

Hii ndio wizara iliyopata fedha kiduchu kuliko wizara zote, licha ya kuwa maeneo inayoyasimamia yanagusa maelfu ya Watanzania wizara hii imepata Sh35.4 bilioni ambapo fedha za maendeleo niSh11.8 bilioni.

Fedha ya shughuli za maendeleo kwenye Wizara hii ni sawa na asilimia 0.04 ya Bajeti Kuu ya Serikali katika miradi ya maendeleo ambayo zaidi ya Sh15 trilioni.

katika , mwaka wa fedha wa 2022/23 ambao unaisha Juni 30, 2023 wizara hii iliidhinishiwa jumla ya Sh35.4 bilioni ambapo kwa mwaka ujao wa fedha imeongezeka Sh19 bilioni pekee huku fedha za maendeleo zikipungua kwa asilimia 25.

2. Ofisi ya Makamu wa Rais Muungano na Mazingira

Licha ya zaidi ya Sh1 bilioni kuongezeka kwenye  bajeti ya wizara hii kwa  mwaka 2023/24 bado inasalia kuwa miongoni mwa wizara zilizopata bajeti kidogo ikiwa na Sh54.1 bilioni.

Miongoni mwa majukumu inayopanga kutekeleza ni pamoja na usimamizi wa mazingira pamoja na kupunguza uharibifu wake, kuimarisha usimamizi wa biashara ya kaboni nchini, na kutoa elimu kwa umma kuhusu hifadhi na usimamizi wa mazingira.


Soma zaidi:


3.Wizara ya Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wanawake na Makundi Maalum

Ikiwa ni bajeti yake ya pili tangu kuanzishwa kwake wizara hii imeidhinishiwa kutumia Sh74.2 bilioni kwa mwaka 2023/24 ambapo ambapo Sh43.6 bilioni ni matumizi ya kawaida huku Sh30.5 bilioni kwa ajili ya miradi ya maendeleo. 

Wizara hii imemegwa kutoka Wizara ya Afya ambapo kutokana na wingi wa shughuli zinazoigusa jamii mwaka 2021 Rais wa Tanzania Samia Suluhu Hassan aliona ni vema kuitenganisha na afya ambayo nayo ni kubwa. 

Vipaumbele vyake katika utekelzaji wa bajeti hiyo ni pamoja na kuratibu na kuwezesha upatikanaji wa haki za watoto na huduma za ustawi wa jamii kwa wazee na kuimarisha mifumo ya malezi, ulinzi na maendeleo ya watoto na familia.

4.Wizara ya Madini

Bunge liliidhinishia Wizara ya Madini Sh89.3 bilioni ili kutekeleza majukumu yake katika mwaka ujao wa fedha utakaonza Julai 2023.

Mipango ya Serikali ni kuiwezesha wizara hiyo kuongeza mchango wake katika pato la taifa mpaka kufikia asilimia 10.

Katika vipaumbele vyake Wizara ya Madini  inatajaria kutekeleza baadhi ya  kuimarisha ukusanyaji wa maduhuli, kuendeleza madini muhimu na madini mkakati,  na kuwaendeleza na kusogeza huduma za ugani kwa wachimbaji wadogo

Vingine ni kuhamasisha shughuli za uongezaji thamani madini, kuhamasisha uwekezaji na biashara katika Sekta ya Madini, pamoja na uanzishwaji wa minada na maonesho ya madini ya vito.

5. Wizara ya Uwekezaji, Viwanda na Biashara

Licha ya umuhimu wake katika kuendeleza uchumi wa viwanda kupitia uwekezaji mkubwa na mdogo wizara hii imepewa Sh119 bilioni pekee kwa ajili ya kufanikisha shughuli zake.

Hata hivyo katika fedha hizo zaidi ya asilimia 50 itatumika kwenye matumizi ya kawaida ambapo Sh75.4 bilioni ni matumizi ya kawaida na Sh43.5 bilioni ndio zitazumika kwa ajili ya matumizi ya maendeleo.

Waziri Ashatu kijazi amesema baadhi ya vipaumbele katika mwaka huu mpya wa fedha ni kuimarisha uwezo wa uzalishaji viwandani na utoaji huduma, kuboresha mazingira ya biashara, kukuza uwezeshaji wananchi kiuchumi na kukuza Sekta binafsi.

 

Kamati za Bunge hazikuridhika

Pamoja na kwamba Bunge limeidhinisha kiwango hicho cha fedha kwa wizara, Kamati za Bunge zinazosimamia kila wizara husika hazikukubaliana na namna Serikali inavyotoa fedha kiduchu kwa wizara hizo kwa kuwa jambo hilo linakwamisha utekelezaji wa shughuli za maendeleo.

Mathalani Kaimu Mwenyekiti wa Kamati ya Bunge ya Elimu, Utamaduni na Michezo Husna Juma Sekiboko aliyekuwa akisoma uchambuzi wa bajeti ya Wizara ya Utamaduni Sanaa na Michezo  aliwaambia wabunge kuwa kamati hiyo haijaridhishwa na kitendo cha Serikali kutoa asilimia 45 tu ya bajeti iliyoidhinishwa kwa mwaka 2022/23 pamoja na kupunguza bajeti ya maendeleo kwa mwaka 2023/24.

“Kamati haijaridhishwa na hatua ya Serikali kupunguza bajeti ya miradi ya maendeleo, hatua hii haiendani kabisa na nia ya Serikali hususani maelekezo ya Rais wa Tanzania Samia Suluhu Hassan ya kukuza na kuimarisha sekta ya utamaduni na sanaa nchini  na haiakisi muamko wa Watanzania ya kupenda na kukumbatia sekta hii muhimu,” alisisitiza Sekiboko.

Jumla ya fedha ambazo Wizara hizi tano zimeidhinishiwa yaani Sh372 bilioni ni sawa na nusu ya bajeti ya Wizara ya Maliasili na Utalii ambayo ni Sh654.6 bilioni.

Enable Notifications OK No thanks