Tanzania kujenga chuo cha Tehama kikubwa Afrika Mashariki
- Chuo hicho kitahusika na utafiti na ubunifu wa teknolojia.
- Kitaisaidia kuwaendeleza vijana wabunifu na kutoa ajira.
- Rais Samia awataka vijana kutumia Tehama kujiletea maendeleo.
Dar es Salaam. Rais wa Tanzania, Samia Suluhu Hassan amesema Serikali ina mpango wa kujenga chuo cha Tehama ambacho kitakuwa cha kwanza na kikubwa katika ukanda wa Afrika Mashariki na Kusini mwa Afrika.
Chuo hicho kikuu kitakuwa kinahusika na kufanya tafiti na ubunifu wa masuala ya teknolojia ya mawasiliano na habari au Tehama.
“Serikali inalenga kujenga chuo kikubwa cha Tehama. Tutatoa kipaumbele kwenye masuala ya utafiti na ubunifu kwenye Tehama. Chuo ambacho nadhani kwa Afrika Mashariki na Kusini mwa Afrika, Tanzania itakuwa inaongoza,” amesema Rais Samia.
Rais Samia ameeleza mipango hiyo ya Serikali leo Oktoba 14, 2021 katika kumbukizi ya miaka 22 ya kifo cha Baba wa Taifa, Mwalimu Julius Nyerere, wiki ya vijana na kilele cha mbio za mwenge wa uhuru zilizofanyika katika Wilaya ya Chato mkoani Geita.
Licha ya kujenga chuo hicho, amesema Serikali itawatambua na kuwasajili vijana wote wanaojihusisha na Tehama.
“Mtakumbuka kwenye hotuba yangu ya vijana pale Mwanza niliwasihi vijana waungane na kushirikiana na kuwa Serikali inatambua vijana wengi wajasiriamali na wabunifu walioanzisha startups (kampuni zinazochipukia) na tech hubs (vituo vya teknolojia) na hivyo Serikali itaangalia namna ya kuwawezesha zaidi ili muweze kukua na kuwa wabunifu wa kimataifa,” amesema Rais.
Kwa sasa, dunia ipo kwenye mapinduzi ya nne ya viwanda ambapo shughuli nyingi zinafanyika kwa kutegemea Tehama ikiwemo kilimo, uvuvi, ufugaji, viwanda, uchimbaji madini, biashara, utoaji wa huduma kama vile afya na elimu.
Kwa kutambua umuhimu wa Tehama, kiongozi huyo mkuu wa nchi amesema Serikali imeondoa kodi ya Ongezeko la Thamani (VAT) kwenye simu janja, vishikwambi na modemu ili kuwajengea vijana mazingira ya kujiajiri kwa maendeleo yao.
“Licha ya faida ya Tehama, ikitumika vibaya inaweza kusababisha madhara makubwa ikiwemo mifarakano, vurugu, machafuko, vita na pia kuongezeka vitendo viovu kama vile wizi, ugaidi, utakatishaji fedha na kadhalika,” amesema Rais huku akiwataka vijana kutumia Tehama kujiletea maendeleo na si vikinginevyo.
Latest