Rais Samia: Mwalimu Nyerere ametuachia wajibu kujenga Taifa la haki
Vijana wakiwa wameubeba mwenge wa Uhuru juu, Chato mkoani Geita leo. Picha| Ikulu.
- Asema ndiyo sababu kubwa ya kuadhimisha siku ya kifo chake.
- Asema alikuwa kiongozi shupavu, jasiri na mwenye maono.
- Mwalimu Nyerere alifariki dunia Oktoba 14, 1999.
Dar es Salaam. Rais Samia Suluhu Hassan amesema kumbukizi ya miaka 22 ya kifo cha Baba wa Taifa, Mwalimu Julius Nyerere inatoa wajibu kwa wananchi na Serikali kutambua na kuyaendeleza mema aliyoyaacha na kuweka mikakati endelevu ya kujenga Taifa imara linalothamini haki na usawa wa watu wake.
Hayati Mwalimu Nyerere alizaliwa mwaka 1922 na kufariki dunia Oktoba 14, 1999 katika hospitali ya Mtakatifu Thomas nchini Ungereza alipokuwa akipatiwa matibabu.
Hata hivyo, falsafa na hotuba zake zimeendelea kuishi ndani na nje ya Tanzania.
“Siku ya leo inatuwezesha kama nchi kuangalia kwa makini tulikotoka, kuchambua tulipo na kuweka mikakati endelevu ya kwenda tunakotaka. Ndugu wananchi leo sote tunawajibika kuyakumbuka mema yaliyofanywa na Baba wa Taifa Mwalimu Julius Nyerere na urithi aliotuachia,” amesema Rais Samia.
Rais Samia alikuwa akizungumza leo Oktoba 14, 2021 katika kumbukizi ya miaka 22 ya kifo cha Baba wa Taifa, Mwalimu Julius Nyerere, wiki ya vijana na kilele cha mbio za mwenge wa uhuru zilizofanyika katika Wilaya ya Chato mkoani Geita.
Amesema Mwalimu Nyerere alikuwa kiongozi wa kipekee kuwahi kutokea siyo tu hapa barani Afrika bali duniani kwa ujumla.
“Alikuwa kiongozi mahiri, jasiri, shupavu, mwenye maono na mwanapinduzi mwanamajumuhi halisi wa Afrika.
“Alikuwa kiongozi bora asiyependa kuwabagua watu kwa sababu yoyote ile iwe dini, kipato, maumbile, itikadi au hata utaifa wake. Na haya ndiyo yaliyotupelekea Serikali kutunga sera zinazoendana na maono yote hayo,” amesema Rais Samia.
Sambamba na uongozi bora, Rais Samia amesema Mwalimu aliwajali wananchi wanyonge ambao walitakiwa kukombolewa kutoka katika madhila yasiyo haki, dhuluma na uonevu.
Kiongozi wa mbio za Mwenge wa Uhuru Kitaifa mwaka 2021 Luteni Josephine Paul Mwambashi akikabidhi Mwenge Maalum wa Uhuru kwa Rais wa Tanzania na Amiri Jeshi na Mkuu wa Majeshi ya Ulinzi na Usalama, Samia Suluhu Hassan. Picha\ Ikulu.
Kiongozi huyo mkuu wa nchi amemtaja Mwalimu Nyerere kuwa aliamini yeye kama kiongozi alihitaji kuongoza Taifa linalojitegemea na ndiyo maana alijitahidi kujenga Taifa lenye kuthamini utu, haki na usawa wa binadamu.
Kupitia jumuiya ya kimataifa, Mwalimu Nyerere alisimama kidete kupinga ubaguzi wa rangi na utawala wa wachache na kazi hiyo kubwa aliyoifanya ndiyo iliyofanya Tanzania kuheshimika ulimwenguni.
Amesema kwa kuzingatia hayo yote, Watanzania wana kila sababu ya kuendelea kumshukuru, kumkumbuka, kumuenzi na pia kuadhimisha siku ya leo ya kifo chake.
“Serikali itendelea kudumisha mambo yote mazuri aliyotuachia baba wa Taifa. Nasema tutajitahidi nikitambua Mwalimu Nyerere ni kigezo cha uongozi bora hapa Tanzania, barani Afrika na duniani,” amesema Rais.
Hata hivyo, Rais Samia ameweka angalizo kuwa kuendeleza falsafa ya Mwalimu Nyerere kunahitaji utulivu, hekima na busara ya kutosha.
Latest
