Waokoaji waendelea kuwatafuta watu 14 waliopata ajali ya ndege Comoro

February 28, 2022 2:20 pm · Mwandishi
Share
Tweet
Copy Link
  • Ndege hiyo ilikuwa na abiria 12 na marubani wawili.

Dar es Salaam. Vikosi vya uokoaji nchini Comoro bado vinaendelea kuwatafuta watu 14 ambao walipata ajali ya ndege mwishoni mwa juma lililopita nchini humo kutokana na sababu zinazodhaniwa kuwa hali mbaya ya hewa.

Kwa mujibu wa mamlaka za Comoro ajali hiyo ilitokea wakati ndege ndogo aina ya Cessna Caravan ilipokuwa ikisafiri kutoka mji mkuu wa Moroni kwenda Fomboni.

Mkurugenzi Mtendaji wa Kampuni ya Fly Zanzibar inayomiliki ndege hiyo Mohammed Mazrui ameiambia Nukta Habari (nukta.co.tz) kuwa walikuwa wamekodisha ndege hiyo kwa kampuni ya Comoro wiki moja iliyopita kwa kipindi cha miezi mitatu.

Mazrui, ambaye yupo nchini Comoro akiungana na vikosi vya uokoaji, amesema ndege hiyo ilikuwa na abiria 12 na marubani wawili.

Vyombo vya habari vya Comoro vinabainisha kuwa kati ya watu 14 walikuwa kwenye ndege hiyo, 12 ni raia wa Comoro na wawili ni Watanzania.

Kampuni ya Fly Zanzibar hutoa huduma za safari za ndege hasa kwa huduma za kitalii nchini Tanzania.

“Hakukuwa na changamoto zozote za kiufundi katika ndege hiyo,” amesema Mazrui kwa njia ya simu na kuongeza “ila hali ya hewa ilibadilika kinyume na matarajio.”

Mazrui amesema kuwa hadi mchana wa Jumatatu Februari 28, 2022 wakiwa angani waliona vipande wanavyohisi kuwa mabaki ya ndege hiyo aina ya Cessna Caravan iliyosajiliwa Tanzania.

Amesema wamekuwa wakitumia ndege hiyo tangu 2016 na haikuwa kuwa na hitilafu yeyote ya kiufundi.

Follow Us on TikTok

FOLLOW NOW

Subscribe to Our YouTube Channel

SUBSCRIBE NOW