Wanaonunua pamba kinyemela kuwajibishwa

May 13, 2022 11:04 am · Mariam John
Share
Tweet
Copy Link

Baadhi ya watumishi wa serikali na wananchi walipotembelea moja ya shamba la pamba katika kijiji cha Mahaha wilayani Magu. Msimu wa ununuzi wa pamba 2021/22 utazinduliwa Mei 20 katika kijiji hicho. Picha |Mariam John.


  • Serikali yawataka wasubiri msimu wa ununuzi uanze.
  • Ni wale wanaonunua pamba shambani.

Mwanza. Bodi ya Pamba Tanzania (TCB) imewaonya wafanyabiashara wanaojipenyeza kinyemela kuwarubuni wakulima wa zao la pamba na kuwauzia bidhaa hiyo kwa bei ndogo ambayo haijaelekezwa Serikali.

Mkurugenzi wa Huduma za Usimamizi TCB, James Shimbe ametoa onyo hilo leo Mei 2022 wakati akizungumza na wakazi wa Kijiji cha Mahaha wilayani Magu, sehemu ambayo uzinduzi wa ununuzi wa zao hilo kitaifa katika msimu huu itatangazwa.

Mkurugenzi huyo amesema zipo taarifa kutoka kwa wananchi kuwa wapo wanunuzi wa zao hilo ambao wameanza kununua kinyemela kabla msimu huo haujatangazwa.

“TCB tumebaini mbinu za walaghai walioanza kununua zao hilo kinyemela na kwamba tunawafuatilia ili hatua kali za kisheria zichukuliwe dhidi yao,” amesema Shimbe.

Shimbe ametumia fursa hiyo kuwaonya kuacha mara moja kuwadhulumu wananchi na kwamba wasubiri hadi kiongozi mwenye dhamana atakayezindua msimu huo.

Katika msimu huu wa 2021/22 zaidi ya tani 21,000 za pamba zitanunuliwa. 

Akizungumzia suala hilo, Mkuu wa Mkoa wa Mwanza, Mhandisi Robert Gabriel amesema bei ya soko la pamba katika msimu huu imeimarika.

“Mei 20 mwaka huu bei ya ununuzi wa zao hilo itatangazwa hivyo niwaombe wawe wavumilivu na wasiruhusu pamba kununuliwa kinyemela kabla ya bei kutangazwa,” amesema Mhandisi Gabriel

Amesema wakulima wametumia nguvu na gharama kubwa kwenye kilimo cha zao hilo hivyo hawatalifumbia macho suala la matapeli watakaowarubuni.


Soma zaidi:


Mkulima katika Kijiji hicho, Bakari Juma amesema  baada ya kufuata maelekezo ya upandaji wa mbegu za pamba kisasa mavuno yameongezeka.

Amesema katika msimu wa kilimo uliopita alivuna kilo za pamba 1,154 na kwa mwaka huu anatarajia kuvuna zaidi ya kilo 1,500.

“Mavuno haya yameongezeka kutokana na kufuata maelekezo ya wataalamu wa kilimo ambapo tulikuwa tunapanda 60 kwa 30 kwa mstari hali ambayo imeongeza mavuno na mafuno yamekuwa makubwa,” amesema Juma.

Hata hivyo, Shimbe amesema kulima kwa namna hiyo kunaongeza tija na mavuno kwa wakulima ambapo kabla ya kuanza kupanda 60 kwa 30 ambapo miche inakuwa zaidi ya 44,000 kwa ekari tofauti na miaka iliyopita ambapo walikuwa wanapanda 90 kwa 40 ambapo miche ilikuwa inafikia zaidi ya 22,000.

Follow Us on TikTok

FOLLOW NOW

Subscribe to Our YouTube Channel

SUBSCRIBE NOW