Majaliwa atoa maagizo mazito pikipiki za maafisa ugani
- Aagiza pikipiki zilizopo wizarani wapewe maafisa hao.
Dar es Salaam. Waziri Mkuu Kassim Majaliwa ametoa siku kwa Wizara ya Kilimo iwe imeondoa pikipiki zote katika ofisi za wizara hiyo zilizopo jijini Dodoma na kuzikabidhi kwa wakurugenzi wa halmashauri nchini.
Majaliwa aliyekuwa akikagua Ofisi za Wizara ya Kilimo zilizopo eneo la VETA, Dodoma na kukuta pikipiki zilizotolewa kwa ajili ya maafisa ugani zikiendelea kuwepo, amesema kuanzia leo Juni 8, 2022 hadi Juni 12, 2022 pikipiki hizo ziwe zimeondolewa kwa sababu zimekaa muda mrefu.
“Hii haikubaliki, Wakurugenzi wote waandikiwe barua waje wazichukue, kama kuna ufungaji wa plate number utafanyika huko huko. Jumapili saa 10 jioni ziwe zimefika kwa wahusuka,” amesema Majaliwa.
Aprili 4, 2022, Rais Samia Suluhu Hassan alizindua ugawaji wa vitendea kazi vilivyoandaliwa na Wizara ya Kilimo kwa ajili ya maafisa ugani wote nchini. Vifaa ni pamoja na pikipiki.
Amesema tayari Rais Samia alishazikabidhi kwa ajili ya kupelekwa kwa maafisa ugani, hivyo kitendo cha pikipiki hizo kuendelea kubaki katika eneo hilo hakikubaliki.
Naibu Katibu Mkuu wa Wizara ya Kilimo, Profesa Siza Tumbo amemuhakikishia Waziri Mkuu kwamba wamepokea maelezo hayo na watayafanyia kazi.
Latest
