Viadudu milioni 9 kumaliza uharibifu zao la pamba Tanzania
- Vitasaidia kuua wadudu wanaharibu pamba.
- Viadudu hivyo vimesambazwa katika mikoa 17.
Mwanza. Huenda wakulima wa pamba wakaongeza uzalishaji na tija kwenye kilimo baada ya wabunifu kuja na teknolojia ya kisasa inayoangamiza wadudu wanaoharibu zao hilo.
Bodi ya Pamba Tanzania (TCB) kwa kushirikiana na Kituo cha Utafiti wa Kilimo Ukiriguru Mkoani Mwanza wamekuja na suluhisho la kukabiliana na wadudu waharibifu baada ya kusambaza viadudu zaidi ya milioni 9 kwenye mikoa 17 inayolima zao la pamba.
Mikoa hiyo ni pamoja na Mwanza, Simiyu na Shinyanga.
Mkurugenzi wa Huduma za Usimamizi TCB), James Shimbe amesema uwepo wa wadudu hao unachangiwa na mabadiliko ya tabianchi hali inayosababisha uzalishaji wa zao hilo kuwa duni.
“Miaka ya nyuma aina hii ya wadudu hawakuwepo, ila kutokana na mabadiliko ya tabiaNCHI wameanza kuonekana kushambulia zao hilo hivyo kufanya uzalishaji kuwa mdogo,” amesema Shimbe.
Shimbe alikuwa akizungumza kwenye Maonyesho ya Sikukuu ya Wakulima Nane Nane kanda ya Magharibi yanayoendelea katika viwanja vya Nyamhongolo jijini Mwanza.
Amesema mbali na kupeleka viuwadudu hao kwa wakulima, lakini pia wanatumia mikakati mbalimbali kuhakikisha zao la pamba linazalishwa kwa tija.
Ametaja moja ya mikakati hiyo ni kutoa elimu kwa wakulima ya umuhimu wa kupanda miche kwa kufuata kanuni bora za kilimo.
Kwa sasa mkulima anatakiwa kupanda kwa sentimita 60/30 ambapo kwa shamba la hekari moja litakuwa na miche 44,444 kutoka miche 22, 222 iliyokuwa inapandwaa kwa sentimita 90/40 kwa shamba kama hilo.
“Pia kupitia balozi wa uhamasishaji wa zao la pamba , Agrey Mwanri anahamasisha wakulima wanafahamu matumizi sahihi ya unyunyizi wa viuatilifu, lakini pia kuhakikisha anapata kwa wakati viatilifu ili kuweza kupambana na wadudu waharibifu,” amesema Shimbe.