Rais Samia azindua kiwanda kikubwa cha vioo Afrika Mashariki
- Vijana zaidi ya 1,000 kupata ajira
- Kitazalisha tani 700 za vioo
Dar es Salaam.Rais wa Tanzania Samia Suluhu Hassan amezindua kiwanda cha kuzalisha vioo kilichopo katika wilaya ya Mkuranga mkoani Pwani kinachotarajiwa kutoa ajira kwa watanzania zaidi ya 1,000.
Kiwanda hicho kilichozinduliwa leo Septemba 20,2023 ni cha nne kwa ukubwa barani Afrika kikitarajiwa kuzalisha tani 700 za vioo kwa siku zitakazotumika katika nchi zote za Afrika Mashariki na kati.
Rais Samia aliyekuwa akizungumza wakati wa uzinduzi wa kiwanda hicho amesema kikikamilika kitawezesha uzalishaji wa bidhaa nyingine kama vioo vya magari na kuchangia kuongezeka kwa pato la taifa.
“Asilimia 75 ya bidhaa zitakavyozalishwa hapa zitauzwa nje ya nchi na kuiletea taifa letu fedha za kigeni hii inamanisha kuwa kiwanda hiki kitakuwa chanzo kikubwa cha fedha hizo za kigeni,” amesema Rais Samia.
Awali Waziri wa Viwanda na Biashara Dkt. Ashatu Kijaji amewaambia wahudhuriaji wa hafla hiyo kuwa kiwanda hicho kikikamilika kitatengeneza ajira zaidi ya 1,650 kwa vijana.
“Kiwanda hiki kimetengeneza ajira za watoto wa kitanzania 750 lakini tutakapo hitimisha kuwekeza kwenye laini zote tatu tutaweza kuajiri watoto wa kitanzania 1,650,” amesema Waziri Kijaji.
Kwa mujibu wa kitabu cha hali ya uchumi kwa mwaka 2022 kinachotolewa na Ofisi ya Taifa ya Takwimu (NBS) sekta ya viwanda imeajiri wafanyakazi 354,477 nchi nzima.
Kati ya idadi hiyo, wafanyakazi 16,634 sawa na asilimia 4.6 wanatoka mkoa wa Pwani wenye jumla ya wakazi 2.02 milioni.
Huenda fursa za ajira zitakazopatikana katika mkoa huo zikaongeza upatikanaji wa huduma nyingine muhimu kama barabara, hospitali, masoko na shule.
Tanzania kuimarisha mifumo ya uwekezaji
Katika kuimarisha na kuboresha huduma za uwekezaji nchini, Serikali inatarajia kuzindua mfumo wa kieletroniki wa kuhudumia wawekezaji (Tanzania electronic investment window) utakaowezesha wawekezaji kupata huduma za usajili kwa haraka.
Mfumo huo unaotarajia kuzinduliwa na Waziri Mkuu Kassim Majaliwa Septemba 25 mwaka huu utaunganisha taasisi 12 zinazotoa huduma kwa wawekezaji hali inayotajwa kupunguza mlolongo mrefu iliokuwa ukilalamikiwa awali.
“Wawekezaji wanaopenda kuanza biashara Tanzania watapewa msaada lkatika masuala muhimu kama usajili wa kampuni, upatikanaji wa ardhi vibali leseni na huduma mbalimbali muhimu kupitia dirisha moja la huduma kwa wawekezaji,” amesema Rais Samia.
Aidha, Rais Samia ameziagiza Wizara na taassis za Serikali zinazohusika na masuala ya uwekezaji kutoa ushirikiano zaidi ili kuvutia uwekezaji nchini.