Zaidi ya Sh699.3 milioni zitakavyopunguza tatizo la usonji Kanda ya Ziwa
- Fedha zinahitajika ili kujenga kituo cha kuwahudumia wenye usonji.
- Kituo hicho kitawapunguzia mzigo wazazi kuwalea watoto hao.
Mwanza. Huenda wazazi wanaowahudumia watoto wenye usonji katika mikoa ya Kanda ya Ziwa wakapata ahueni baada wadau wa maendeleo kuandaa mpango wa kuwasaidia watoto hao kupata huduma muhimu ili kuwawezesha kutimiza ndoto zao.
Taasisi isiyo ya kiserikali inayoshughulikia ya Living Together Foundation (Li-Tafo) imeanzisha kampeni kabambe ya kuchagisha fedha zaidi ya Sh699.3 milioni kwa ajili ya ujenzi wa kituo cha utoaji huduma za usonji mkoani Mwanza.
Mtoa huduma wa Li- TAFO, James Mushi amesema kupitia uzoefu wao wa kushughulikia masuala ya usonji wamebaini kuwa ipo idadi kuba ya watoto na vijana wenye changamoto ya usonji Kanda ya Ziwa.
Amesema matarajio yao baada ya kukamilika kwa kituo hicho kitatoa huduma za usonji katika nyanja mbalimbali zikiwemo afya, mazoezi ya tabia, vitendo na kuzungumza. Pia kitatoa elimu na ushauri kwa wazazi walezi na jamii.
“Changamoto nyingine tuliyoibaini ni uelewa mdogo kwa jamii kushughulikia tatizo hilo, lakini pia upatikanaji wa huduma ni chache ambapo wenye uhitaji hulazimika kuzifuata Moshi na Dar es Salaam,” amesema Mushi.
Mushi ameeleza kuwa katika shule nyingi jumuishi hazina mazingira rafiki ya kukidhi mahitaji ya watu wenye usonjim hivyo wameona kuna umuhimu wa kuwa kituo kwa ajili ya watoto wenye changamoto hiyo ya kiafya.
Zinazohusiana:
-
Mama aacha kazi kumlea mwanae mwenye usonji
-
Falsafa ya michezo kuboresha elimu, afya ya watoto
-
VIDEO: Jinsi maziwa ya mama yanavyoimarisha afya ya mtoto
Serikali mkoani Mwanza imewapatia tayari kiwanja kwa ajili ya ujenzi wa kituo hicho.
“Tunaiomba Serikali kutilia mkazo suala hili la kiwanja, pia tunaomba wadau na jamii kutushika mkono kwa kuchangia gharama za ujenzi ambazo ni zaidi ya Sh 699.3 milioni ili watoto waweze kupata huduma karibu,” amesema Mushi.
Awali Mhadhili Msaidizi wa Chuo cha Sebastian Kolowa Memorial (SEKOMU), Alfred Walalaze amesema kumekuwepo na mitazamo hasi kwa jamii ambayo inachukulia mtu mwenye usonji au mlemavu wa akilii ni kama mzigo na asiyestahili kupatiwa huduma muhimu na wengine.
Amesema ili kuondoa changamoto hizo ni vema kuwapatia elimu wazazi na jamii kukubali kuwa ulemavu ni mapenzi ya Mungu na kuwaelekeza mahali pa kupata msaada ikiwemo vituo vya afya, shule na hospitali.
Mkuu wa Wilaya ya Magu, Salum Kali amesema ofisi ya Mkuu wa Mkoa wa Mwanza haitakua kikwazo katika kuwapatia kiwanja ili kuhakikisha kinajengwa kituo kitakachowahudumia watoto wenye usonji.
“Serikali itashirikiana na Li-TAFO kuhakikisha ujenzi wa kituo unafanikiwa na ni mipango ya Serikali kuhakikisha watoto wenye usonji wanaishi kama watoto wengine,” amesema Kali.
Latest
