Zaidi ya Sh3 bilioni kupunguza uhaba wa maji Kilimanjaro
- Miradi saba ya maji itatekelezwa kupitia fedha hizo na kusaidia wananchi kupambana na Uviko-19.
Dar es Salaam. Wizara ya Maji ilipewa kiasi cha Sh139.4 bilioni ili kutekeleza miradi 218 katika halmashauri mbalimbali nchini, fedha hizo zikiwa ni sehemu ya mkopo wa dharura uliotolewa na Shirika la Fedha Duniani (IMF) kwa Tanzania.
Mkopo huo ambao ni Dola za Marekani milioni 567.25 (Sh1.3 trilioni) ulitolewa kwa ajili ya kukabiliana na athari za ugonjwa wa Corona (Uviko-19), kwa kutatua changamoto za huduma za kijamii ikiwemo afya, elimu na maji.
Kwa mujibu wa wizara ya maji upatikanaji wa huduma ya maji nchini umeongezeka katika miaka ya hivi karibuni na kufikia asilimia 72% mwezi Juni 2021 kutoka asilimia 64.8 mwaka 2019 kwa upande wa vijijini.
Katika maeneo ya mijini wastani wa upatikanaji wa maji safi na salama umeongezeka na kufikia asilimia 86 mwaka 2021.
Licha ya ongezeko hilo, siyo maeneo yote nchini yamefikiwa na huduma za maji, jambo linaloleta changamoto kwa watu kukidhi mahitaji ya shughuli mbalimbali.
Utolewaji wa fedha hizo utasaidia kuboresha miundombinu ya upatikanaji wa maji na kusaidia wananchi kupambana na athari za Uviko-19.
Kati ya fedha hizo Mkoa wa Kilimanjaro umepata Sh3.47 bilioni kutekeleza miradi saba ya maji ya safi na salama.

Latest