Waziri Ummy: Ebola ni hatari lazima tuchukue hatua
- Amesema ugonjwa huo umefika jijini Kampala na Entebbe, nchini Uganda.
- Muingiliano wa Tanzania na Uganda unaweza kuibua mlipuko nchini.
- Serikali yajipanga kuudhibiti usiingie nchini.
Dar es Salaam. Licha ya kuwa Tanzania bado haijaripoti mgonjwa yeyote wa Ebola, Waziri wa Afya Ummy Mwalimu amesema nchi iko hatarini kupata ugonjwa huo kutoka Uganda kutokana na mwingiliano wa watu, shughuli za kiuchumi na kijamii.
Amesema ni vyema hatua madhubuti za udhibiti wa ugonjwa huo zikachukuliwa haraka kwa sababu ugonjwa wa Ebola ni tishio.
Waziri Ummy amesema hadi kufikia Oktoba 29, 2022 katika nchi ya Uganda ambapo kuna ugonjwa wa Ebola wamepata wagonjwa wapya 5 na kufanya idadi ya waliopata maambukizi hayo tangu mlipuko kufikia watu 126.
Waliolazwa 54 na vifo 32 vimethibitika huku wataalam wa afya wakifuatilia watu 2,183 ambao walikuwa karibu na watu waliothibitishwa kuwa na ugonjwa huo.
“Wasiwasi wetu unazidi baada ya kuwa ugonjwa umeingia Kampala na Entebbe kwa ndege zinazokuja kutoka Kampala, kuja Dar es Salaam na mabasi,” amesema Ummy.
Amesema kuibuka kwa Ebola nchini Uganda kunaiweka Tanzania katika hatari ya kupata mlipuko huu Kutokana na mwingiliano mkubwa wa kiuchumi na kijamii na Uganda.
Soma zaidi:
Hatua zinazochukuliwa kudhibiti ugonjwa huo
Waziri Ummy amesema timu ya wataalam ya kukabiliana na magonjwa ya mlipuko itapatiwa mafunzo ya namna ya kukabiliana na ugonjwa wa ebola ili waweze kutoa huduma bora.
Jana Oktoba 30, 2022 alitembelea Mkoa wa Dares Salaam kuangalia utayari wa kukabiliana na wagonjwa wa #Ebola endapo tutapata wagonjwa huku akiridhishwa na kiwango cha maandalizi yaloyofanywa na mkoa huo.
“Hata hivyo bado tunahitaji kuongeza nguvu katika baadhi ya maeneo hususani ya kutoa mafunzo kwa Timu za Haraka za Dharura za kukabiliana na ugonjwa huu, kuongeza vifaa kinga na pia kutoa elimu kwa wananchi kuhusu dalili za ugonjwa huu na njia za kujikinga,” amesema Ummy.
Ugonjwa huo ni miongoni mwa magonjwa yanayosambaa kutoka kwa wanyama kwenda kwa binadamu kwa kula au kugusa mnyama mwenye maambukizi kama nyani, kima, popo na swala.
Ebola inaenea kutoka kwa binadamu mmoja kwenda kwa mwingine kwa kugusa majimaji ya mwili wa mgonjwa kwa mfano mate, machozi, damu, matapishi, mkojo na kinyesi. Endapo mtu ataona dalili hizi awahi kituo cha kutolea huduma za afya.
Aidha, Waziri Ummy amewaomba wadau wa maendeleo kuiunga mkono Tanzania ili iweza kujiandaa vyema na kukabiliana na Ebola endapo itaingia nchini.
“Shirika la Afya Duniani (WHO) limeahidi kuleta nchini Tanzania wataalamu ambao waliwahi kutoa matibabu kwa wagonjwa wa Ebola ikiwamo huko Liberia,” amesema Ummy na kusisitiza kuwa hadi sasa Tanzania haina mgonjwa wa Ebola.