Wasamaria wajitokeza kuwasaidia wanafamilia waliokatwa miguu kwa “ugonjwa wa ajabu”

March 16, 2021 5:07 am · Mariam John
Share
Tweet
Copy Link
  • Wameanza kupatiwa miguu ya bandia kuwawezesha kuendelea na shughuli zao.
  • Ni familia inayoongozwa na Amina Kalazi (60) mkazi wa kijiji cha Igayaza wilayani Muleba ambayo imekumbwa na ugonjwa uliofanya watu saba wa familia yake kukatwa miguu.
  • Madaktari bado wanasugua vichwa kubaini chanzo cha ugonjwa huo. 

Mwanza. Siku chache baada ya Nukta Habari kufanya ripoti maalum iliyoangazia kuhusu familia ya watu 10 waliokatwa miguu kutokana na “ugonjwa wa ajabu”, baadhi ya wanafamilia hao wameanza kupata misaada ikiwemo kupewa miguu bandia itakayowawezesha kuendelea na shughuli zao.

Pia madaktari katika Hospitali ya Rufaa Kanda ya Ziwa Bugando jijini Mwanza wanaendelea kufanya uchunguzi juu ya ugonjwa huo na namna nzuri ya kuipatia matibabu familia hiyo.

Familia hiyo ni ya Amina Kalazi (60) mkazi wa kijiji cha Igayaza wilayani Muleba ambayo imekuwa ikitawaliwa na machozi baada ya kukumbwa na ugonjwa uliofanya watu saba wa familia yake kukatwa miguu.

Kwa sasa Amina anaishi katika mtaa wa Lumala jijini Mwanza pamoja na baadhi ya wanawe baada ya kupata msamaria mwema ili kutafuta suluhu ya tatizo linalowakabili. 

Huenda historia ya Amina na familia ikabadilika baada watu mbalimbali kujitokeza ili kuwasaidia kurudi katika hali ya kawaida ikiwemo kuwasaidia kupata miguu ya bandia na matibabu.

Mkurugenzi wa taasisi ya Nitetee, Flora Lauwo ambaye anaishi na familia hiyo ameiambia Nukta Habari (www.nukta.co.tz) kuwa tayari imepatikana miguu mitatu bandia ambayo amepatiwa Amina na watoto wake wawili Rahma Kilanzi na Husna Athuman ambao miguu yao ilikatwa.

“Watatu walifanikiwa kupata miguu bandia wiki iliyopita kutokana na michango ya watu mbalimbali,” amesema Flora wakati akitoa mrejesho wa misaada inayotolewa kwa familia hiyo.

Flora ambaye ni mjasiriamali na mwanaharakati wa masuala ya kijinsia amesema miguu hiyo mitatu imegharimu zaidi ya Sh4.5 milioni na imetengenezwa katika Hospitali ya Rufaa Kanda ya Ziwa Bugando jijini Mwanza. 

Amesema baadhi ya watu wametoa vyakula na dawa ili kuisaidia familia hiyo huku akiiomba jamii na Serikali kuisaidia familia hiyo ambayo inahitaji msaada wa matibabu.


Soma zaidi: 


Madaktari waanza kuchunguza ugonjwa huo wa ajabu

Daktari Bingwa  wa mifupa kutoka hospital ya Bugando, Inyasi Akaro amesema bado hawajabaini tatizo la familia hiyo kukatwa miguu na wanaendelea kufanya uchunguzi wa kisayansi ili kubaini ugonjwa huo wa ajabu. 

“Pamoja na vipimo vyote bado hatujafikia mwafaka kuona aina ya ugonjwa unaowasumbua,  na kwa bahati mbaya tunachangamoto ya ukosefu wa maabara zinazoweza kupima magonjwa ya ndani (Genetics),” amesema Dk Akaro. 

Tayari wataalam hao wa afya wamechukua vipimo vya familia hiyo ili kuendelea na uchunguzi wao kwa sababu mpaka sasa hakuna viashiria vyovyote vya ya ugonjwa wanaoweza kuufananisha kwa kuwa unatokea kwa gafla kama miiba,  funza  na ngozi kubadilika damu na wanapofika hospitali hubaini sehemu ya vidole vya miguu inakuwa imekufa. 

 Dk Akaro anaeleza kwa undani kuhusu hatua inayofuata kuwasaidia wanafamilia hao. Tazama video hii kufahamu zaidi. 

                               

Follow Us on TikTok

FOLLOW NOW

Subscribe to Our YouTube Channel

SUBSCRIBE NOW