Waanzisha kampeni kulinda haki za wanawake, kumiliki ardhi
- Kampeni hiyo ya Stand for her land imezinduliwa na shirika lisilo la kiserikali la Landesa na mashirika mengine 25
- Itasaidia kujua wanawake walio na matatizo katika umiliki ardhi Tanzania.
Dar es Salaam. Huenda tatizo la umiliki ardhi linalo wakumba wanawake wengi kwenye jamii zetu za Kitanzania likapungua, baada ya Shirika lisilo la Kiserikali Landesa kwa kushirikiana na mashirika mengine 25 nchini Tanzania kuzindua kampeni ya kulinda haki za mwanamke kwenye umliki wa ardhi.
Kampeni hiyo iliyopewa jina la Stand For her Land (Linda ardhi ya mwanamke) inakusudia kuelimisha wanawake wa Kitanzania juu ya haki walizonazo katika umiliki wa ardhi ili kusaidia kupunguza tatizo hilo.
Kazi kubwa ya kampeni hiyo, ni kuangazia wanawake wenye matatizo ya ardhi na kutumia njia sahihi ili kuhakikisha jamii mbalimbali za Tanzania zina neemeka na umiliki ardhi kwa wanawake .
Stand For her Land imeanza kufanya kazi nchini Tanzania toka kuzinduliwa kwake Novemba 21,2019 kwa kuanzia kwa mkoa wa Dar es Salaam, mbali na kampeni hiyo pia inatoa suluhisho kwa kina mama waliotharika na tatizo hilo katika maeneo mbali mbali nchini.
“Kampeni hii inafanya kazi kulinda haki za wanawake duniani kote kwa kuziba pengo lililopo kati ya sheria na utekelezaji kwa kuhakikisha kuna usawa kwa jamii zote Tanzania,” Inaeleza Landesa katika tovuti yao Stand4herland.org.
Zinazohusiana:
Pia Landesa inafanya kazi kwa ushirikiano na mashirika mengine yasiyo ya kiserikali yapatayo 25 ikiwemo Tamwa na Fahamu Sheria Foundation inayoendesha programu tumishi ya Sheria Kiganjani.
Kupitia program hiyo tumishi hadi sasa kampeni hiyo imeweza kuwafikia wanawake 357 na inasaidia kujua wanawake walio na kesi za umiliki ardhi zinazoendelea na ziilizoisha.
“Kwa asilimia kubwa programu tumishi hii inatusaidia kuratibu mchakato huu kwa urahisi ili kuhakikisha tunafikia wanawake wengi zaidi,” amesema Brian Malya mwakilishi kutoka Sheria Kiganjani.