Vyakula vya kuepuka kujilinda na ugonjwa ya figo
- Ni pamoja na vyakula vyenye kiasi kikubwa cha protini, chumvi na kalsiamu.
Dar es Salaam. Ugonjwa wa figo ni miongoni mwa magonjwa yasiyo ya kuambukiza yanayozidi kuongezeka duniani, yakichangia vifo vya mamilioni ya watu duniani kote.
Takwimu zinaonesha asilimia saba ya Watanzania wanaugua ugonjwa sugu wa figo, ukiwathiri zaidi wakazi wa mjini kwa asilimia 15 kulinganisha na asilimia mbili za wakazi wa vijijini.
Awali ugonjwa huu uliripotiwa zaidi kwa wazee wenye umri wa zaidi miaka 45, lakini miaka ya hivi karibuni maradhi hayo yamekuwa yakishambulia watu wa rika zote ikichangiwa zaidi na mtindo mbovu wa maisha.
Vifuatavyo ni vyakula na vinywaji ambavyo vinatakiwa kuepukwa au kupunguzwa ili kujilinda na ugonjwa wa figo.
Vyakula vyenye mafuta mengi
Ulaji uliopitiliza wa mafuta mengi, hasa yale mabaya (saturated fats), huongeza mzigo na kuzorotesha afya ya figo.
Mafuta haya hupatikana zaidi kwenye bidhaa kama siagi na samli pamoja na aina nyingine za mafuta ya mbegu yasiyo salama.
Mratibu wa Tiba na Magonjwa Yasiyoambukiza katika Halmashauri ya Manispaa ya Kinondoni, Dk Omari Mwangaza, anasisitiza umuhimu wa wananchi kuzingatia aina ya mafuta wanayotumia katika mapishi yao ya kila siku.
“Mafuta mazuri ni yale yenye omega-3, omega-6 au omega-9, ikiwa mafuta yako hayana hizo yana madhara,” anaeleza Dk Mwangaza.
Omega -3 ni mafuta ambayo yanapatika kwenye vyakula kama samaki wa bahari, 0mega-6 (alizeti) na omega-9 (mzaituni na parachichi) yakisaidia kulinda afya ya moyo na kuboresha ustawi wa mwili kwa ujumla.
Vyakula vyenye chumvi (sodium) nyingi
Madini ya sodium yana jukumu la kudhibiti kiwango cha maji mwilini. Hata hivyo, yakizidi huweza kusababisha maji kubaki mwilini na kuleta madhara kama vile kuvimba kwa mwili, shinikizo la damu, uzito kuongezeka ghafla na matatizo ya kupumua.
Vyakula vyenye sodium nyingi ni pamoja na nyama iliyohifadhiwa kwa chumvi, samaki waliokaushwa kwa chumvi, soseji na ‘bacon’ ambazo wataalamu wa afya wanazitaja kuwa chanzo cha magonjwa ya figo.
Dk Mwangaza ameshauri kudhibiti vyakula vya chumvi kwa sababu milli ya watu wenye asili ya kiafrika huwa na mwitikio mkubwa zaidi katika matumizi ya chumvi na sukari
Mtaalamu huyo wa afya amewarai Watanzania kujenga tabia ya kutoongeza chumvi mezani wakati wa kula chakula.
Unywaji wa maji/vinywaji venye sukari kupitiliza
Ingawa maji ni muhimu kwa mwili, kunywa kupita kiasi kunaweza kuwa na madhara hata kwa watu wenye figo zenye afya.
Figo hufanya kazi ya kusafisha damu na kudhibiti maji na madini mwilini, na unywaji wa maji mengi huongeza mzigo na kupunguza ufanisi wa kawaida.
Tovuti ya Medical News Today inasema kuwa mbali na madhara ya moja kwa moja katika figo, unywaji wa maji mengi unaweza kushusha kiwango cha sodiamu kwenye damu (hyponatremia),kusababisha uchovu, maumivu ya kichwa,au matatizo ya fahamu kwa muda mfupi.
Mbali na maji, Dk Mwangaza anaeleza kuwa unywaji wa vimiminika vingine vyenye sukari ikiwemo pombe zenye sukari kupitiliza huchochea uzalishaji wa sukari isiyohitajika kwenye mwili wa binadamu jambo linaloweza kumletea mtumiaji matatizo ya figo.
Vyakula vyenye protini nyingi
Protini inapovunjwa vunjwa mwilini hutengeneza mabaki kama vile urea, amonia na ‘creatinine’.
Kwa mtu mwenye matatizo ya figo, mabaki haya huweza kuongezeka na kuathiri zaidi utendaji wa figo.
Hivyo ni muhimu kupunguza ulaji wa protini nyingi na kuchagua protini zinazotumiwa kwa ufanisi zaidi na mwili, kama vile mayai, samaki, nyama, kuku, maziwa na jibini.
Vyakula vyenye protini ambazo huacha mabaki mengi ni pamoja na mbogamboga, matunda, maharage, kunde, mbaazi, mahindi, mtama, karanga, mkate.
Latest