Vitabu vya sauti: Rafiki wa safari yako
- Vitakusaidia kusoma vitabu vingi kwa wakati mmoja huku akifurahia safari yako.
- Vitakupunguzia uchovu na kukufanya ufurahie mandhari nzuri ya nchi ukiwa njiani.
- Lakini unahitaji kuchukua tahadhari hasa unapotumia “earphone” kusikiliza vitabu.
Dar es Salaam. Raha ya safari bwana ni kufurahia kila kitu kinachokuja mbele ya macho yako. Naam! Unaweza kushangaa jirani yako anasema ameona twiga huku wewe ulichokiona ni usingizi au maneno unayoyasoma kwenye kitabu chako.
Kwa macho yako ndipo utaona tamaduni za jamii unazopishana nazo ukiwa safarini, miti mikubwa mithiri ya mwili wa tembo na hata nyumba zilizoezekwa kwa ustadi mkubwa na zikipambwa na mapambo asili kama magamba ya konokono na zingine zikiota nyasi kwenye paa.
Hata hivyo, kusoma vitabu ni hulka ya baadhi ya watu wanapokuwa safarini kwani ni muda wa utulivu na usio na bugudha lakini mara nyingi wanajikuta wakishindwa kufanya utalii murua kwa kuzingatia kinachoendelea nje ya basi au gari wanalosafiria.
Uchambuzi wa Nukta (www.nukta.co.tz) umegundua kuwa unaweza kupata maudhui ya kitabu chako kwa mfumo wa sauti (Audiobooks) na hizi ndizo faida utakazozipata kwa kuchagua kusikiliza kitabu chako badala ya kukisoma.
Utapata nafasi ya kufurahia mazingira ambayo yapo njiani kuelekea sehemu uendapo.
Unaachaje kuufurahia uzuri wa mito, mabonde, milima ambayo unakutana nayo safarini kuelekea sehemu uendapo? Kupitia kusikiliza kitabu chako, utapa wasaa wa kufuatilia vitu kama hivyo ambavyo huenda hukuwahi kuvifahamu hapo awali.
Unaposoma kitabu, inakulazimu kuweka umakini wako wote kwenye ukurasa lakini endapo utasikiliza, macho yako yanaweza kufurahia uzuri uliopo nje ya basi lako. Picha| Digital trends.
Pia, itakupunguzia uwezekano wa kupata adha mbalimbali zinazotokana na kusoma kitabu kwenye simu yako kwa muda mrefu zikiwemo kuumwa kichwa na kupoteza umakini kwenye usomaji wako.
Ndiyo, ni mara ngapi umeacha kusoma kitabu na kuingia kwenye mtandao wa kijamii kujibu meseji za wadau? Kama unasikiliza kitabu, utaepukana na adha hizo na kukufanya upate maarifa yaliyokusudiwa.
Mbali na hilo, kusikiliza kitabu chako badala ya kusoma itakuongezea nafasi kwenye begi lako ambayo utaitumia kuweka vitu vingine vya muhimu zikiwemo nguo na kupunguza uzito wa begi.
Zaidi, wapo watu ambao wakishika kitabu na usingizi unaanza kuwanyemelea. Kwa kusikiliza vitabu, kuna uwezekano wa wewe kumaliza vitabu vingi zaidi kwani ni kama unavyosikiliza muziki. Unachohitaji ni “earphones” za masikioni ambazo zitakuondolea kumsumbua jirani yako kwa sauti asiyoihitaji.
Zinazohusiana
- Hivi ndivyo unavyoweza kufanya utalii ukiwa angani Tanzania
- Hii ndiyo safari unayoweza kuifanya ndani ya chumba chako
- Corona ilivyoathiri shughuli za utalii duniani
Hata hivyo, unahitaji kuwa makini na epuka kutumia ear/headphone kwa muda mrefu huku sauti ya ukiwa umeiseti hadi mwisho ili kulinda masikio yako.
Kufahamu juu ya madhara ya vifaa hivyo kwa vijana wengi soma hapa.
Zaidi na changaoto za kiafya, huenda ukapitwa na matangazo ambayo yanaweza kutolewa kwenye gari na hata kushindwa kuchangamana na jirani yako.
Muhimu tenga muda utakaosikiliza kitabu na baada ya hapo endelea na mambo mengine.
Pia, kupata vitabu hivi itakulazimu utoboe mfuko kidogo kwani kupitia tovuti ya Audiobooks, vitabu hivyo vinalipiwa takriban Sh34,000 kwa kifurushi cha mwezi ambapo unaweza kupata vitabu zaidi ya 100,000 vya kusoma.
Latest