Vipaumbele saba Wizara ya Utamaduni, Sanaa na Michezo 2022-23
- Kukuza shughuli za michezo, sanaa na utamaduni nchini.
- Wizara hiyo inapanga kutumia Sh35.4 bilioni.
Dar es Salaam. Wizara ya Utamaduni, Sanaa na Michezo imesema katika mwaka wa fedha 2022/23 imepanga kutekeleza vipaumbele saba ikiwemo kujenga, kukarabati na kuboresha miundombinu ya tamaduni, anaa na michezo nchini.
Waziri Mohammed Mchengerwa aliyekuwa akiwasilisha makadirio ya bajeti ya wizara hiyo kwa mwaka huo amesema itatumia Sh35.4 bilioni ambapo ikilinganishwa na bajeti ya 2021/22 imeshuka kutoka Sh54.7 bilioni.
Kushuka kwa bajeti hiyo huenda ni kwa sababu wizara hiyo iligawanywa kutoka Wizara ya Habari, michezo, Sanaa na Utamaduni na hivyo majukumu kupungua.
Hata hivyo, hadi kufikia mwezi Mei, 2022 Wizara hiyo imepokea Sh34.3 bilioni sawa na asilimia 85.6 ya bajeti yote ya mwaka huu unaoisha Juni 30.
Vipaumbele saba vya wizara hiyo
Waziri Mchengerwa amesema kuwa wizara hiyo imejipanga kuratibu, kuendesha na kusimamia matamasha na matukio makubwa ya utamaduni, sanaa na michezo.
“Wizara itaendelea kuimarisha, kuziwezesha na kufanikisha ushiriki wa Timu za Taifa katika michezo na michuano mbalimbali,” amesema waziri huyo.
Soma zaidi:
Vilevile, kuhamasisha wadau kusaidia timu, vilabu na wawakilishi mbalimbali wa kitaifa katika ushiriki wa michezo na michuano ya kimataifa.
Maeneo mengine ni kukamilisha mikakati, miongozo na kanuni mbalimbali za kisera na kisheria katika kuimarisha usimamizi na utekelezaji katika sekta za utamaduni, sanaa na michezo.
Amesema watajenga, kuimarisha na kuongeza uwezo wa kitaasisi katika usimamizi na utekelezaji wa masuala ya sekta za utamaduni, sanaa na michezo.
“Tutaimarisha ushirikiano na wizara 22 nyingine katika utendaji kazi hususani zile zinazohusika na masuala ya kazi na ajira; Tamisemi, Elimu, Afya, Maliasili na Utalii, Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki,” amesisitiza.
Pia kuimarisha ushirikiano na wadau mbalimbali ikiwemo sekta binafsi katika maendeleo ya sekta za utamaduni, sanaa na michezo.
Licha ya Serikali kuonyesha nia ya dhati kuendeleza michezo nchini, Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Huduma na Maendeleo ya Jamii imeishauri kuendelea kuwekeza zaidi katika sekta hiyo kwa kuiongezea bajeti wizara hiyo ili itekeleze kazi zake kwa ufanisi.
“Wakati bajeti kuu ikiongezeka hali inayoleta matazamo chanya wa maendeleo ya nchi, kwa ujumla bajeti namba 96 inaendelea kupungua hali hii inaleta taswira hasi katika maendeleo ya wizara hii,” amesema Stanslaus Nyongo Mwenyekiti wa kamati hiyo.
Latest
