Vifahamu vitabu 16 vilivyozuiliwa kutumika shuleni Tanzania
- Vitabu hivyo vimekutwa katika baadhi ya shule.
- Vinadaiwa kukinzana na mila na desturi za Watanzania.
Dar es Salaam. Waziri wa Elimu, Sayansi na Teknolojia Profesa Adolf Mkenda amepiga marufuku matumizi ya vitabu 16 vya ziada kutumika katika shule za umma na binafsi Tanzania kikiwemo “Diary of a Wimpy Kid.”
Waziri Mkenda ametoa marufuku hiyo leo Februari 13, 2023 kwa mamlaka aliyopewa chini ya kifungu 59 cha Sheria ya Elimu Sura 353.
Vitabu vya 16 vilivyopigwa marufuku vimekutwa katika baadhi ya shule si kama vitabu vya kiada wala ziada ambapo maudhui yake yanakinzana na mila, desturi na utamaduni wa Mtanzania na yanahatarisha ukuaji wa wanafunzi.
“Shule zinakumbushwa kufuata mwongozo wa Waraka wa Elimu Na wa kuwa vitabu vyote vya ziada vinavyoandikwa na waandishi binafsi vinatakiwa kuwa na ithibati ya ubora inayotolewa na Kamishna wa Elimu,” amesema Mkenda.
Vitabu vilivyopigwa marufuku kutumika na kuwepo shuleni ni Diary of a Wimpy Kid, Diary of a Wimpy Kid -Rodrick Rules, Diary of Wimpy Kid-The Last Straw, Diary of Wimpy Kid-Dog Days, Diary of a Wimpy Kid The Ugly Truth na Diary of a Wimpy Kid -Cabin Fever.
Vingine ni Diary of a Wimpy Kid – The Third Wheel, Diary of a Wimpy Kid – Hard Luck, Diary of a Wimpy Kid – The Long Haul, Diary of a Wimpy Kid -Old School, Diary of a Wimpy Kid -Double Down, Diary of a Wimpy Kid-The Gateway, Diary na Diary of a Wimpy Kid-Diper Overlode.
Vitabu vingine vilivyopigwa marufuku kutumika shuleni ni Is for TANSGENDER (You Know Best Who You Are!), Is for LGBTQIA (Find the Words that Make You) na Sex Education a Guide to Life.
Baada ya kutolewa kwa marufuku hiyo kumekuwa na mjadala mpana kuhusu vitabu hivyo huku baadhi ya watu wakisema ni uamuzi mzuri kwa sababu utasaidia watoto kuendeleza utamaduni wa Mtanzania.
“Hongera Waziri wa Elimu na Wizara kwa ujumla kwa kuhakikisha hakuna agenda ya siri inayoingizwa kwa watoto wetu ambayo ni kinyume na maadili yetu, jambo lingine ni kuthibiti baadhi ya channels za TV ambazo zinafundisha maadili isiyokubalika,” ameandika mtumiaji wa Twitter, Saimon Mosingo.
Hata hivyo, baadhi ya watumiaji mtandaoni wamesema Waziri alipaswa kuweka wazi utamaduni na mila ambazo watu wanatakiwa kuzifuata kuliko kupiga marufuku vitabu hivyo.
Latest
