TRA kuwaweka kitanzini watumiaji wa namba za magari zisizotambuliwa

October 6, 2022 2:36 pm · Mwandishi
Share
Tweet
Copy Link
  • Yabaini baadhi ya watu wanatengeneza namba hizo bila idhini.
  • Yasema itachukua hatua kali kwa wahusika. 

Dar es Salaam. Mamlaka ya Mapato Tanzania (TRA) imesema itachukua hatua kali za kisheria kwa wamiliki wa magari wanaotumia namba ambazo hazijatolewa na mamlaka hiyo. 

Hatua hiyo imekuja baada ya TRA kubaini uwepo wa magari barabarani yaliyobandikwa na kutumia namba ambazo haijazitoa au kutolewa na taasisi nyingine za Serikali ambazo zimepewa jukumu hilo kisheria.

“Aidha, kumekuwepo na matumizi ya vibati vya namba vyenye rangi zisizotambulika kisheria vinavyowekwa mbele na nyuma ya vyombo vya moto (Plate number),” imesema TRA katika taarifa yake iliyotolewa leo Oktoba 6, 2022.

TRA imesema utengenezaji na matumizi ya vibati hivyo ni kosa kisheria kama inavyoelezwa kwenye Kifungu cha 8 cha Sheria ya Usalama Barabarani (The Road Traffic Act, 1973).

“Hatua kali za kisheria zitachukuliwa kwa yeyote anayekiuka sheria hii ikiwa ni pamoja na kutaifisha chombo cha moto husika,” imesisitiza mamlaka hiyo.

Kwa mujibu wa Wizara ya Fedha na Mipango, kila chombo cha moto kinachosajiliwa katika mfumo mpya wa kuandikisha magari kinapewa namba mpya katika utaratibu wa tarakimu na herufi mfano T 100 AAA. 

Herufi T inamaanisha nchi ya Tanzania ikifuatiwa na tarakimu tatu na herufi tatu ambazo zinatofautiana utambulisho wa gari moja na gari jingine. 

Mfumo huo umelisaidia Jeshi la Polisi kupata taarifa muhimu hususani wakati wa uhalifu kutambua gari husika limesajiliwa kwenye kituo gani, wakati gani na linamilikiwa na nani.

Kila gari linalosajasiliwa Tanzania huwa na namba maalum. Picha | Daudi Mbapani.

“Taarifa hizi husaidia Jeshi la Polisi kufuatilia gari iliyohusika katika tukio na kuchukua hatua zinazostahili. Utaratibu huu wa kuwa na mtengenezaji mmoja wa vibao vya nambari za usajili hutumika pia na nchi kama Kenya na Sweden,” alieleza alieyekuwa Naibu Waziri wa Fedha, Abdisalaam Khatib Bungeni Novemba 9, 2006.

Serikali iliamua kumteua mtengenezaji mmoja tu wa vibao vya namba za usajili. Vibao vinatengenezwa kwa mfumo na viwango vya kitaifa na kimataifa kwa maagizo toka kwa Serikali ikisaidiwa na TRA. 

Mtengenezaji huyo ameunganishwa kwenye mtandao wa mfumo mzima wa usajili wa magari ili aweze kufanikisha majukumu yake kirahisi.


Faida za namba za magari

Khatib alisema kutokana na mfumo huu Serikali imeweza kuongeza mapato yake zaidi kwa vile mfumo huu unazuia udanganyifu unaoweza kufanywa na watu ambao si waaminifu.

Pia mefanikiwa kuboresha shughuli za utawala wa kodi katika usajili wa magari, kudhibiti uingizaji holela wa magari bila ya kufuata sheria, kupunguza wimbi la wizi wa magari na kuboresha huduma kwa wenye magari kuondoa usumbufu usiokuwa wa lazima. 

Follow Us on TikTok

FOLLOW NOW

Subscribe to Our YouTube Channel

SUBSCRIBE NOW