Tasac:Uchunguzi wa meli iliyozama Mwanza bado unaendelea
- Yasema tayari imeanza kupokea taarifa za awali kuhusiana na ajali hiyo na uzembe wowote ukibainkka hatua zitachukuliwa.
Mwanza. Shirika la Uwakala wa Meli Nchini (TASAC) limesema bado linaendelea na uchunguzi wa ajali ya meli ya Mv. Claries iliyozama Mei 19, 2024 mwaka huu na iwapo kutabainika uzembe hatua zitachukuliwa.
Mkurugenzi wa Tasac, Mohamed Salum aliyekuwa akizungumza katika kikao kilichokutanisha wadau wa masuala ya usafirishaji wa meli Ziwa Victoria leo Mei 28, 2024, amesema wameshapokea taarifa ya awali kuhusiana na kuzama kwa chombo hicho na tayari wameshaanza kuchukua hatua za kiusalama kuzuia kutokea tena kwa ajali hiyo.
“Kila kukicha tunaendelea kujifunza kuhusiana na matukio yanayotokea kwenye vyombo vya usafiri majini, yapo matukio ambayo yametokea nchini ikiwemo ajali ya mv Bukoba na hata hii ya Mv Claries kama Tasac tutaangalia namna ya kufanya ili kuhakikisha usalama unakuwepo,” amesema Salum.
Taarifa ya Tasac inakuja zikiwa zimepita siku 9 tangu meli hiyo izame katika Ziwa Victoria ambapo bado shughuli ya kuitoa meli hiyo majini inaendelea.
Katika hatua nyingine, Salum amesema kutoka na changamoto hiyo ipo haja ya kuwekeza katika masuala ya uokozi wa vyombo vya majini ili kusaidia pale inapotokea ajali ya ziwa au Bahari.
Naye Afisa Mkuu wa Kampuni ya Huduma za Meli Nchini (MSCL)ameishauri Serikali kuunda Kamati huru itakayosimamia uokoaji pale meli itakapopata changamoto baharini huku akiwatoa hofu wananchi juu ya matumizi ya usafiri huo.
Latest
