Tanzania yapokea msaada wa dawa, vifaa tiba kutoka Misri
- Gharama ya vifaa na dawa hizo ni Sh864 milioni.
- Msaada huo ni matokeo ya ziara ya Rais Samia nchini Misri.
- Serikali ya Misri imeahidi kuendelea kuisaidia sekta ya afya nchini.
Dar es Salaam. Tanzania imepokea msaada wa dawa pamoja na vifaa tiba vyenye thamani ya Sh864 milioni vilivyotolewa na Serikali ya Misri vitavyosaidia katika kupambana na magonjwa mbalimbali nchini.
Msaada huo umetolewa leo Januari 14, 2022 katika uwanja wa ndege wa kimataifa wa Julius Nyerere (JNIA) Jijini Dar es salaam na Balozi wa Misri nchini Tanzania, Mohamed Abouelwafa na kupokelewa na Katibu Mkuu Wizara ya Afya Profesa Abel Makubi kwa niaba ya Waziri wa Afya, Ummy Mwalimu.
Prof Makubi amesema msaada huo umeletwa baada ya ziara ya kikazi ya Rais wa Tanzania, Samia Suluhu Hassan nchini Misri mnamo Novemba mwaka jana.
“Tunamshukuru sana Mheshimiwa Samia Suluhu Hassan Rais wa Jamhuri ya Tanzania pamoja na Serikali ya Misri kwa kushirikiana na Tanzania hasa katika kuboresha Sekta ya Afya kwa kusaidia mahitaji mbalimbali ikiwemo upatikanaji wa dawa na vifaa tiba,” amesema Prof Makubi.
Soma zaidi:
- Rais awatolea uvivu mawaziri, manaibu mawaziri
- Nape aagiza uchunguzi vifo vya wanahabari misafara ya viongozi wa Serikali
- Hoja maboresho sheria ya vyombo vya habari yaibuka tena msibani Mwanza
Prof Makubi amesema msaada huo utaenda kuwasaidia wananchi wenye uhitaji katika vituo mbalimbali vya kutolea huduma za afya nchini.
Tanzania na Misri zimekuwa na ushirikiano wa muda mrefu katika sekta mbalimbali ikiwemo za afya, elimu, uchumi na biashara.
Balozi wa Misri nchini Tanzania, Abouelwafa amesema kujitoa kwa Serikali ya Misri kusaidia sekta ya afya ni kuunga mkono jitihada za Rais Samia katika kuwaletea maendeleo wananchi ikiwemo kuboresha sekta hiyo kwa kupambana na magonjwa mbalimbali.
“Serikali ya Misri itaendelea kushirikiana na Tanzania katika kusaidia maendeleo ya Watanzania, hasa katika kuboresha aekta ya afya,” amesema Balozi Abouelwafa.
Latest