Tanzania kuimarisha huduma za afya ya akili kupunguza vifo vya kujiua
- Kwa mujibu wa Shirika la Afya Duniani (WHO), kila sekunde 40 mtu mmoja duniani hujitoa uhai, ambapo ni sawana takribani watu 800,000 kila mwaka.
Dar es Salaam. Tanzania imeungana na mataifa mengine ulimwenguni kuadhimisha Siku ya Kuzuia Kujiua Duniani, ambayo hufanyika kila mwaka siku kama ya leo yaani Septemba 10, ikiwa na lengo la kuongeza uelewa, kuhamasisha mshikamano wa kijamii na kulinda afya ya akili ya wananchi.
Tanzania hufanya maadhimisho haya kila mwaka, ambapo kwa 2025 kauli mbiu ni “Kuleta Matumaini Kupitia Vitendo,”.
Kwa mujibu wa taarifa iliyotolewa na Mganga Mkuu wa Serikali, Dk. Grace Magembe leo, kauli mbiu hiyo inalenga kuwahimiza wananchi kushirikiana na familia, marafiki, wahudumu wa afya pamoja na viongozi wa dini na siasa kupunguza vifo vinavyotokana na kujiua.
“Huu ni wakati wa kuwezesha wengine kuchukua udhibiti wa maisha yao na kuthamini uhai walionao,” imeeleza taarifa ya Dk Magembe.
Kwa mujibu wa Shirika la Afya Duniani (WHO), kila sekunde 40 mtu mmoja duniani hujitoa uhai, ambapo ni sawana takribani watu 800,000 kila mwaka.
Aidha, kujiua kumeendelea kuwa sababu kuu ya vifo kwa vijana wenye umri kati ya miaka 15 hadi 29, huku kwa kila kifo kimoja kukiwa na majaribio mengine yasiyopungua 40.
Wizara ya Afya imesisitiza kuwa mawazo ya kujiua yanaweza kumpata mtu yeyote, bila kujali umri au nafasi aliyonayo kwenye jamii.
Ikieleza kuwa watu wanaoteseka kisaikolojia wanahitaji msaada na mazingira salama ya kuongea bila kuhukumiwa.
Aidha, wizara imeeleza kuwa inaendelea kuchukua hatua katika mapambano dhidi ya tatizo la afya ya akili, ikiwemo kuimarisha huduma za ushauri nasaha kwenye vituo vya afya, kuanzisha dawati la msaada wa kisaikolojia kupitia simu namba 199 bila malipo na ujumbe mfupi kwenda 15061, pamoja na kutoa mafunzo kwa wahudumu wa afya.
Mikakati mingine ni pamoja na kushirikiana na viongozi wa dini, asasi za kiraia na wadau mbalimbali kuondoa unyanyapaa unaohusiana na matatizo ya akili, na kuhimiza wananchi kutafuta msaada mapema.
“Tunatoa wito kwa jamii nzima kushirikiana kupambana na tatizo hili. Tujifunze kusikiliza bila kuhukumu, kuonesha upendo na huruma kwa wale wanaopitia changamoto za afya ya akili na kuwahimiza kutafuta msaada,” imeeleza taarifa hiyo.
Wizara ya Afya imesisitiza kuwa kila mmoja ana jukumu la kulinda na kuthamini maisha, na ni muhimu kujenga mazingira salama ya kuzungumza wazi bila aibu ili kuondoa unyanyapaa dhidi ya matatizo ya akili.
Latest
