Spika Ndugai: Jimbo la Buhigwe liko wazi

March 30, 2021 11:41 am · Rodgers Raphael
Share
Tweet
Copy Link
  • Ni baada ya Mbunge wa jimbo hilo, Dk Philip Mpango kuteuliwa kuwa Makamu wa Rais wa Tanzania leo.
  • Uteuzi huo unaacha wazi jimbo la Buhigwe la mkoani Kigoma na Wizara ya Fedha na Mipango. watu
  • Spika Ndugai ameitaka NEC na Waziri Mkuu kuanza mchakato wa kujaza nafasi hizo mbili.

Dar es Salaam. Kufuatia Dk Philip Mpango kuteuliwa kuwa Makamu wa Rais wa Tanzania, Spika wa Bunge la Tanzania Job Ndugai ametangaza kuwa jimbo la Buhigwe mkoani Kigoma liko wazi.

Dk Mpango ambaye alikuwa Waziri wa Fedha na Mipango katika Serikali ya Hayati Rais John Magufuli amethibitishwa leo (Machi 30, 2021) kuwa Makamu wa Rais baada ya kupigiwa kura 363 na Wabunge jijini Dodoma.

 “Katiba ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania inatoa maelekezo kuhusu muda wa Wabunge kushika madaraka yao. Ibara ya 71 inaorodhesha mambo ambayo kwayo mbunge atakoma kuwa mbunge na ataacha kiti chake cha ubunge. Miongoni mwa mambo hayo ni iwapo mbunge anachaguliwa au anateuliwa kuwa makamu wa rais,” amesema Spika Ndugai.

Spika Ndugai amesema baada ya bunge kumthibitisha Dk Mpango kuwa Makamu wa Rais mteule leo, imemuondolea sifa ya kuendelea kuwa Mbunge wa jimbo la Buhigwe hivyo ameitaarifu Tume ya Taifa ya Uchaguzi (NEC) kuwa kiti cha ubunge wa jimbo hilo sasa kipo wazi.


Soma Zaidi:


Aidha, Dk Mpango ambaye kitaaluma ni mchumi ataachia nafasi yake ya Waziri wa Fedha na Mipango ambayo ameishikilia tangu mwaka 2015 hadi Rais Magufuli anafariki Machi 17 mwaka huu.

Kutokana na nafasi hiyo nyeti, Spika Ndugai amemuomba Waziri Mkuu Kassim Majaliwa kuangalia uwezekano wa kumpata mtu sahihi aliyesimama hasa kipindi hichi ambacho Bunge linatarajia kuanza kujadili bajeti kuu ya Serikali kwa mwaka 2021/22.

Muda mfupi kabla ya kuthibitishwa na Bunge, Mpango amewashukuru wananchi wa Buhigwe ambao walimchagua kwa kura zaidi ya asilimia 70 katika Uchaguzi Mkuu wa Oktoba mwaka jana na amesema ataendelea kuwa karibu nao kwani Buhigwe ni nyumbani. 

“Nawaombea naamini kabisa watapata mwakilishi mwingine mahiri kwa ajili ya kusemea matakwa yao, shida zao katika Bunge hili,” amesema Dk Mpango akiwasisitiza wabunge wote wa Mkoa wa Kigoma kuendelea kusema matatizo ya wakazi wa mkoa huo bungeni.

Follow Us on TikTok

FOLLOW NOW

Subscribe to Our YouTube Channel

SUBSCRIBE NOW