Serikali yapendekeza kodi mpya kwenye kamari Tanzania
- Pendekezo hilo jipya linatarajia kuingiza Sh74.5 bilioni kwenye kibubu cha Serikali mwaka 2026/27.
Dar es Salaam. Serikali imeendelea kuwakomalia wacheza kamari baada ya kupendekeza kutoza ushuru wa bidhaa kwa kiwango cha asilimia 5 kwenye thamani ya dau la kamari ikiwa ni moja ya hatua ya kudhibiti uraibu wa michezo hiyo inayokua kwa kasi zaidi nchini.
Hatua hiyo mpya ya Serikali ya Rais Samia Suluhu Hassan inatarajia kuongeza mapato ya Serikali kwa kiasi cha Sh74.5 bilioni katika mwaka wa fedha wa 2026/27 unaoanza Julai mwaka huu.
Pendekezo hilo linahusisha michezo ya kamari (gaming) inayochezwa kwa njia ya michezo ya kubashiri ya ardhini au mtandaoni (land/internet based sports betting), michezo ya kasino ya ardhini au mtandanoni (land based/internet casino), mashine za sloti arobaini (forty machine) pamoja na michezo ya vikaragosi (virtual games operations).
Ushuru wa bidhaa ni ushuru unaotozwa kwa bidhaa na huduma maalum zinazozalishwa ndani ya nchi au kuagizwa kwa viwango tofauti.
Waziri wa Fedha wa Tanzania, Balozi Khamis Mussa Omar ameliambia Bunge jijini Dodoma kuwa asilimia 10 au moja ya 10 ya mapato yatakayokusanywa kutoka kwenye chanzo hiki (ushuru wa asilimia 5) yatawasilishwa Bodi ya Michezo ya Kubahatisha (GBT) ili kuongeza ufanisi katika udhibiti wa michezo ya kubahatisha.
“Lengo la hatua hii ni kupunguza madhara yanayosababishwa na michezo ya kubahatisha ikiwemo uraibu na kupungua kwa nguvu kazi ya Taifa kutokana na baadhi ya vijana kujihusisha zaidi katika shughuli hizo badala ya shughuli za kiuchumi,” amesema Omar katika hotuba ya Bajeti Kuu ya Serikali ya mwaka 2026/27 leo Juni 11, 2026.
Kwa mujibu wa Omar, hatua hiyo itaongeza mapato ya Serikali ambayo pamoja na masuala mengine yanatumika katika kugharamia utekelezaji wa shughuli za kiuchumi.
Kwa muda mrefu kumekuwa na shinikizo kubwa kwa Serikali kuendelea kudhibti kamari ikiwemo michezo ya kubashiri maarufu kama betting kutokana na athari kwa vijana. Baadhi ya wakosoaji wamesema kushamiri kwa michezo hiyo kunaongeza uraibu na ni hatari kwa ustawi wa maendeleo nchini kwa kuwa vijana wanawaza kutajirika kwa njia rahisi badala ya kufanya kazi.
Ongezeko la kodi ya ushuru wa bidhaa utapeleka maumivu kwa kampuni za betting na wacheza kamari maarufu kama wakamaria kwa kuwa tayari wamekuwa wakitozwa kodi za michezo ya kubahatisha (Gaming Tax).
Hadi sasa Mamlaka ya Mapato Tanzania (TRA) hutoza kodi mbalimbali kwenye michezo ya kubahatisha zikiwemo kodi ya asilimia 25 ya mapato ghafi (Mauzo baada ya kutoa gharama za ushindi) na 12% ya jumla ya zawadi aliyoshinda mchezaji
kwenye michezo ya kubashiri matokeo (Sports Betting).