Serikali kupiga marufuku uagizaji nyuzi za plastiki, kukuza kilimo cha mkonge
- Serikali yasema huo ni muendelezo wa kupiga marufuku matumizi ya bidhaa za plastiki.
- Amesema hatua hiyo itasaidia kukuza viwanda vya ndani vinavyotengeneza nyuzi za zao la mkonge.
- Itasaidia kutengeneza fursa za ajira kwa Watanzania.
Dar es Salaam. Waziri Mkuu Kassim Majaliwa amesema Serikali itadhibiti uagizaji wa nyuzi za plastiki kutoka nje ya nchi ili kuchochea ukuaji wa viwanda vya ndani vinavyotengeneza bidhaa hiyo kutokana na zao la mkonge.
Hatu hiyo inafuatia swali la Mbunge wa Korogwe Vijijini, Timotheo Mzava aliyehoji juu ya uwekezaji wa viwanda vidogo, vya kati na vikubwa kwa mazao ya kimkakati likiwemo zao la mkonge ili kuchochea maendeleo ya kiuchumi nchini.
Majaliwa akijibu swali hilo leo Februari 4, 2021 katika kipindi cha maswali kwa Waziri Mkuu bungeni amesema kati ya mikakati inayofanywa na Serikali ni pamoja na kuongeza uwekezaji wa viwanda vya ndani na kuboresha teknolojia ya viwanda hasa ambavyo havifanyi kazi kutokana na uchakavu.
“Viko viwanda ambavyo wawekezaji wamejenga vinakwama kupata masoko mazuri kwa sababu kuna bidhaa zisizokuwa na sifa zinazoingia nchini.
“Ili kuendeleza uwekezaji huo, moja kati ya jambo kubwa tunalolifanya ni kuhakikisha kwamba tunadhibiti bidhaa kutoka nje ili kuwezesha uwekezaji wa ndani kukua,” amesema Majaliwa.
Mikakati hiyo ya kudhibiti bidhaa, mtendaji huyo mkuu wa Serikali amesema inahusisha kudhibiti nyuzi za plastiki kutoka nje ya nchi ili kukikuza kilimo cha mkonge.
“Tunacho kiwanda kinazalisha nyuzi nchini kupitia zao la mkonge na kiwanda hiki kinazalisha bidhaa mbalimbali za nyuzi zenye ukubwa tofauti tofauti. Tunazo bidhaa za plastiki zinaingia nchini huku Tanzania tukiwa tumeshazuia kuingiza plastiki,” amesema Majaliwa.
Soma zaidi:
- Maoni mchanganyiko matumizi fedha za Tasaf Mwanza
- Wasafi TV yapunguziwa adhabu, kurudi hewani Machi mosi
- Yakuzingatia kabla hujasaini mkataba wa ajira
Tangu Aprili mwaka jana, Serikali ilianza kutekeleza marufuku ya matumizi ya mifuko ya plastiki inayotumika kufungashia baadhi ya bidhaa ili kupunguza uharibifu wa mazingira.
Waziri Majaliwa amesema kupigwa marufuku kwa matumizi ya plastiki nchini kunaendelea kwa awamu na ilianza na marufuku ya plastiki za kubebea mizigo na zile za viroba.
“Sasa tutakwenda mbali zaidi tunaingia kwenye nyuzi kwa lengo la kumlinda mwekezaji wetu aliyejenga kiwanda nchini lakini pia ambaye anatumia zao letu la mkonge kuzalisha bidhaa mbalimbali ikiwemo na nyuzi,” amesema
Majaliwa amesema kwa kufanya hivyo, Tanzania itanufaika kwa kupata soko zuri, ajira na wakulima kuhamasika kulima zao la mkonge kwa kuwa na uhakika wa soko.
Latest
