Majaliwa: Hatutawatupa wawekezaji
- Asema Serikali itaendelea kufanya nao kazi kwa karibu.
- Uwekezaji unasaidia kupunguza uagizaji wa bidhaa nje ya nchi.
Dar es Salaam. Waziri Mkuu Kassim Majaliwa amesema Serikali itaendelea kufanya kazi kwa karibu na wawekezaji ili kuhakikisha uwekezaji wao haukwami bali unakua na kuleta tija kwa Tanzania.
Waziri Maliwa ameyasema hayo Novemba 28, 2022 alipotembelea na kuweka jiwe la msingi kwenye kiwanda cha kutengeneza mabati cha Lodhia kilichopo Mkuranga mkoani Pwani.
Akizungumza kwenye kiwanda hicho Majaliwa amesema Serikali ina dhamira ya dhati ya kuhakikisha wawekezaji nchini wanapata faida.
“Tunathamini uwekezaji huu, tunaheshimu uwekezaji huu na tutakuunga mkono kwenye uwekezaji,” amesema Majaliwa.
Amesema Serikali inatambua mchango wa wawekezaji katika kuchangia maendeleo ya nchi katika sekta mbalimbali ikiwemo afya, elimu, kilimo, mawasiliano na hata ajira.
“Upanuzi wa kiwanda hiki ni kumuunga mkono Rais Samia katika jitihada zake za kuendelea kupunguza changamoto ya upatikanaji wa ajira kwa Watanzania,” amesema Majaliwa.
Soma zaidi
-
Takriban watu 11 kwa kila 100,000 hujiua kila mwaka Afrika
-
Idadi ya watalii yaongezeka baada ya kushuka kwa miezi miwili mfululizo
Uwepo wa wawekezaji hao kwenye sekta mbalimbali ikiwemo viwanda utasaidia nchi kuwa na uhakika wa upatikanaji wa bidhaa ndani ya nchi badala ya kuagiza kutoka nje pekee.
“Leo hii hatuna haja sana ya kuagiza nondo Ulaya au Asia, nyingi zinapatikana hapa nchini ikiwemo kwenye kiwanda hiki cha Lodhia”
Aidha Waziri Mkuu amewataka wafanyakazi wa kampuni hiyo kuwa mabalozi wazuri kwa kufanya kazi kwa weledi na uaminifu ili kuhakikisha malengo ya muwekezaji yanatimia.
“Endeleni kufanya kazi vizuri kwenye kampuni hii, ninyi ni mabalozi wetu wazuri,” amesisitiza Majaliwa.
Latest