Safari bado ndefu utoaji vitambulisho vya Taifa Tanzania
- Zaidi ya nusu ya waliojisajili hawajapata vitambulisho.
- Kamati yasema kasi ya uzalishaji vitambulisho ni ndogo.
Dar es Salaam. Licha ya zaidi ya Watanzania milioni 23.6 kujisajili katika Mamlaka ya Vitambulisho vya Taifa (Nida) kwa ajili ya kupata vitambulisho vya Taifa au namba ya kitambulisho hicho, zaidi ya nusu bado hawajapata nyaraka hiyo.
Kitambulisho cha Taifa au namba yake ni miongoni mwa nyaraka ambayo huhitajika katika masuala muhimu, kama usajili wa laini za mawasiliano, maombi ya pasipoti, leseni pamoja na huduma mbalimbali kutoka Serikalini.
Vita Kawawa ambaye ni Mwenyekiti Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Mambo ya Nje, Ulinzi na Usalama aliyekuwa akiwasilisha taarifa ya kamati hiyo leo Februari 6, 2023 Bungeni jijini Dodoma amewaambia wabunge kuwa kasi ya uzalishaji wa vitambulisho hivyo ni ndogo ikilinganishwa na mahitaji halisi.
“Uchambuzi wa kamati umebaini kuwa Mamlaka ya Vitambulisho vya Taifa (Nida) imegawa vitambulisho milioni 10.2 pamoja na jitihada mbalimbali bado idadi ya vitambulisho vinavyozalishwa ni ndogo,” amesema Kawawa.
Soma zaidi
-
Ni umri gani sahihi kumpeleka mtoto katika madarasa ya awali?
-
Wizi mafuta reli ya kisasa washika kasi, polisi waingilia kati
Kwa mujibu wa Kawawa mpaka Novemba 2022, Nida ilikuwa imesajili jumla ya watu milioni 23.6 ambapo waliopata namba za vitambulisho ni milioni 19.6 huku waliopata vitambulisho ni milioni 10.2 pekee.
Idadi ya waliosajiliwa ni sawa na asilimia 68 ya lengo la kuwasajili watu milioni 34 ifikapo mwaka 2025/26.
Itakumbukwa Disemba 2022, Nida ilizindua mfumo wa usajili wa watu kwa njia ya mtandao utakaowezesha wananchi wenye sifa za kuomba vitambulisho vya Taifa kwa kujaza fomu mtandaoni.
Kwa mujibu wa Geoffrey Tengeneza ambaye ni Mkuu wa Mawasiliano wa Nida, mfumo huo unawahusu wale ambao wana vifaa vinavyoweza kupokea intaneti kama simu na kompyuta ambapo watalazimika kuingia katika tovuti ya mamlaka hiyo.
Licha ya mfumo huo mpya kutegemewa kupunguza usumbufu, muda na gharama bado unaweza kuwa changamoto kwa watu waishio vijijini ambako hakuna huduma ya intaneti.