Baidu kuongeza ushindani soko la akili bandia
- Kuzindua huduma mpya ya akili bandia Machi 2023.
- Ni hatua ya kukuza mapato na kuongeza ushindani.
Dar es Salaam. Kampuni ya Baidu Inc inapanga kuzindua huduma mpya ya “Chatbot” itakayowezesha watumiaji wake kupata matokeo yaliyochakatwa kwa mfumo wa akili bandia unaofanana na ChatGPT ya OpenAI itakapofika Machi mwaka huu.
Kwa mujibu wa Reuters, zana hiyo ya mtandaoni ambayo bado haijapewa jina itajumuishwa katika huduma kuu za utafutaji wa vitu mtandaoni ya Baidu na kuruhusu watumiaji wake kupata matokeo ya utafutaji kwa mtindo wa mazungumzo kama wa jukwaa maarufu la OpenAI.
Chatbot ni programu ya kompyuta inayotumia Akili Bandia (AI) na uchakataji wa lugha asilia (NLP) kuelewa maswali ya wateja na kuwajibu kiotomatiki na pia kuiga mfumo wa mazungumzo kama ya binadamu.
ChatGPT ni zana mpya ya mtandaoni inayotumia teknolojia ya chatbot inayoendeshwa na akili bandia. Imetengenezwa na kampuni ya OpenAI ya Marekani chini ya Bilioni Elon Musk na Sam Altman.
Zana hiyo ya kidijitali imeundwa kwa kutumia idadi kubwa ya data za wavuti na kuboreshwa kupitia maoni ya binadamu, ujuzi wa kujibu kwa maandishi vidokezo vya watumiaji kwa njia ya asili na ya ubunifu.
Hivi sasa chatbot inayotumika China ni kwaajili ya mawasiliano ya kijamii ilhali ChatGPT inafanya kazi za kitaalam kwa mapana zaidi kama vile kupanga programu na kuandika insha.
Soma zaidi:
Baidu inapanga uboreshaji kwa kujumuisha matokeo yanayotokana na maneno ya watumiaji wanapotuma maombi ya utafutaji, badala ya viungo (links) pekee.
Baidu imekuwa ikiwekeza kwa kiasi kikubwa katika teknolojia ya akili bandia kama vile huduma za wingu (cloud services), utengenezaji chipu, na uundaji wa magari yawezayo kujiendesha na hivi karibuni kuongeza huduma za uandishi wa skrini, uchoraji na uhariri.
Wakati taarifa hii inadokezwa tayari kampuni kubwa ya kompyuta ya Microsoft hivi karibuni imetangaza uwekezaji mkubwa wa Dola za Marekani bilioni 10 kama ishara ya ukuaji wa kasi wa teknolojia inayotumia zana za akili bandia.
Pia imeongeza programu ya kuunda picha ya OpenAI kwenye injini yake ya utafutaji ya Bing kama changamoto mpya ya ushindani dhidi ya kampuni ya mama ya Google, Alphabet Inc.
Kwa Baidu kuingia katika soko la akili bandia inaamanisha kuongezeka kwa ushindani na motisha ya kukuza ujuzi wa ChatGPT na teknolojia zinazofanana, huku ikitafuta kubadilisha na kuongeza vyanzo vyake vya mapato.
Latest



