Rais Samia: Wakuu wa wilaya fanyeni kazi msisubiri ‘mkeka’

September 30, 2022 9:55 am · admin
Share
Tweet
Copy Link
  • Awataka waache kusubiri “mkeka’ mpya kwani hakusema atawabadilisha. 
  • Asisitiza wakuu wa mikoa kupeleka ripoti ya utendaji ya wakuu wa wilaya.

Dar es Salaam. Rais wa Tanzania Samia Suluhu Hassan amewataka wakuu wa wilaya zote nchini kutimiza majukumu yao ipasavyo na kuacha kusubiri orodha mpya ya wakuu wa wilaya.

Rais Samia amewaambia wakuu wa wilaya waliokuwepo kwenye hafla ya utiaji saini  Mkataba wa Usimamiaji wa Shughuli za Lishe  jijini Dodoma leo Septemba 30, 2022 kuwa amepata taarifa za baadhi yao kutofanya kazi ipasavyo na kusubiri orodha ya wateule wapya.

“Napata meseji huku hawafanyi kazi wapo kama wamepigwa ganzi. Nilisema tulichofanya ni uchambuzi wa utendaji wenu tumjue nani mzuri nani mbaya, aliyesema anataka kuwabadilisha nani?,” amesema Rais Samia.

Mwezi Julai mwaka huu Rais Samia alifanya mabadiliko ya baadhi ya wakuu wa mikoa nchini kwa wengine kuhamishiwa viituo na baadhi kuondolewa kabisa.


Soma Zaidi 


Rais Samia amesisitiza kuwa yeye ndiyo mwenye jukumu la kufanya mabadiliko kwa wakati atakaoona unafaa na hivyo amewaagiza wakuu wa mikoa kupeleka ripoti ya utendaji wa wakuu wa wilaya.

‘Wakuu wa mikoa nataka ripoti ya wakuu wenu wa wilaya, aliyepigwa ganzi nani mwenye nusu kaputi nani, kama hawawezi tutoe tuweke wengine,” amesisitiza Rais Samia.

Sambamba na maagizo hayo wakuu wa wilaya wametakiwa kusimamia ipasavyo utekelezaji wa mikataba ya lishe ambayo imesainiwa hii leo Septemba 30 katika jengo la kitega uchumi jijini Dodoma kwa kushirikiana na wakuu wa mikoa.

Baadhi ya mambo yanayotakiwa kusimamiwa kwenye mikataba ya lishe ni kusimamia ulaji wa chakula bora, matibabu ya utapiamlo mkali, matumizi ya dawa za kuongeza virutubisho pamoja na huduma za unasihi katika ngazi za jamii na zahanati.

Follow Us on TikTok

FOLLOW NOW

Subscribe to Our YouTube Channel

SUBSCRIBE NOW