Rais Samia: Nimetengua zuio la mikutano ya hadhara vyama vya siasa
- Ni baada ya kutofanyika kwa kipindi cha zaidi ya miaka mitano.
- Asisitiza kufanya siasa za kistaarabu na kujenga nchi.
- Marekebisho mengine ya sheria na kukwamua mchakato wa katiba yanaendelea.
Dar es Salaam. Rais wa Tanzania Samia Suluhu Hassan ameruhusu mikutano ya hadhara ya vyama vya kisiasa kuendelea kufanyika nchini, huku akiwaasa wanasiasa kufanya siasa za kistaarabu na za kujenga nchi.
Marufuku ya mikutano ya hadhara ya kisiasa iliwekwa na aliyekuwa Rais wa awamu ya tano wa Tanzania Hayati John Pombe Magufuli mwaka 2016 akiwataka watu kufanya kazi na kusubiri mpaka muda wa uchaguzi ndipo wafanye mikutano hiyo.
Rais Samia aliyekuwa akizungumza katika mkutano wake na viongozi wa vyama 19 vyenye usajili wa kudumu kuwa kufanya mikutano ya hadhara ni haki hivyo yeye kama Rais anaruhusu mikutano hiyo ianze kufanyika.
“Uwepo wangu leo mbele yenu ni kuja kutoa ruhusa, kuja kutangaza kwamba lile tangazo la kuzuia mikutano ya hadhara sasa linaondoshwa, …. ni haki kwa vyama vya siasa kuendesha mikutano ya hadhara, “ amesema Rais Samia huku akipigiwa makofi.
Ruhusa hiyo ya mikutano ya hadhara inakuja ikiwa imepita miezi miwili tangu Rais Samia alipopokea mapendekezo ya kikosi kazi cha kuratibu na kuchakata maoni ya wadau wa demokrasia na kuahidi kuyafanyia kazi ambapo suala la mikutano ya siasa ni miongoni mwa mambo yaliyopewa kipaumbele.
Itakumbukwa baadhi ya viongozi wa vyama vya upinzani nchini Tanzania wamewahi kujikuta katika mikono vya vyombo vya dola kwa kukiuka katazo hilo ambalo lilipingwa vikali na wadau wa demokrasia kuwa linakiuka Katiba ya nchi.
Pamoja na ruhusa hiyo, Samia amewakumbusha viongozi wa kisiasa kufanya siasa za kistaarabu, kujenga nchi pamoja na kuzingatia kanuni na sheria za nchi bila kusahau mila na desturi za kitanzania.
“Ndugu zangu tuna wajibu, kwa upande wa Serikali tumeshajipanga wajibu wetu ni kuwalinda mfanye mikutano yenu salama, wajibu wenu vyama vya siasa ni kufuata sheria na kanuni,
“Twendeni tukafanye siasa za kistaarabu za kupevuka, kujenga na si kubomoa, si kurudi nyuma, tusiende kutukanana, hiyo sio mila na desturi zetu, “ amesema Samia kwa msisitizo.
Rais Samia amesema ili kuijenga Tanzania moja bado wanaendelea na mchakato wa kubadilisha baadhi ya sheria pamoja na kuukwamua mchakato wa Katiba ili kuona njia gani itafaa katika kupata Katiba Mpya.
Habari hii imeandikwa na Esau Ng’umbi
Latest
