Rais Samia asisitiza kudumisha usalama, umoja, amani nchini
- Asema haitawezekana kuligawa/kuuza au kuharibu amani yaTaifa.
- Askofu Shoo amtaka aendelee kutumia hekima kufanya maamuzi.
Dar es Salaam. Rais Samia Suluhu Hassan amewataka Watanzania kuendelea kudumisha usalama, umoja, na amani kwa ajili ya maendeleo ya Tanzania na kuongeza kuwa kamwe haitawezekana kwa mtu au kikundi cha watu kuligawa Taifa.
Rais Samia aliyekuwa akizungumza katika maadhimisho ya miaka 60 ya Kanisa la Kiinjili la Kilutheri Tanzania(KKKT) leo Agosti 21, amewaambia wahudhuriaji kuwa amekuwa akikaa kimya hata pale anaposikia kauli za maudhi na ataendelea kukaa kimya.
“Niliamua kunyamaza kimya na naendelea kunyamaza kimya, ninachotaka kuwahakikishia hakuna mwenye misuli na ubavu wa kuligawa Taifa hili, wa kuuza taifa hili, wa kuharibu amani na usalama tuliojenga kwenye taifa hili, huu ndio ujumbe wangu kwenu,” amesema Rais Samia jijini Arusha.
Ujumbe huo wa Rais Samia, unatokana na hotuba ya Askofu Mkuu wa kanisa la KKKT Dk.Fredrick Shoo aliyemuomba Rais Samia kutumia hekima katika kukabiliana na ukosoaji wa mkataba wa ushirikiano wa uendeshaji wa bandari kati ya Tanzania na Dubai unaoendelea.
Soma zaidi
-
Rais Samia awataka mabalozi kufanya kazi kwa matokeo, si matukio
-
Rais Samia:Mashirika ya Umma jiendesheni kwa faida
Itakumbukwa tangu Bunge la Tanzania lilipopitisha azimio la ushirikiano wa uendeshaji wa bandari kati ya Tanzania na Dubai, makundi mbalimbali wakiwemo wanasiasa, wanasheria pamoja na wanaharakati yamekuwa yakiibuka kuukosoa mkataba huo huku wengine wakitaka ufutwe kabisa.
Hata hivyo, Dk. Shoo amebainisha kuwa wao kama viongozi wa dini walishakutana na Rais na kumweleza mapungufu ya kufanyiwa kazi kwenye mkataba huo ambapo Rais Samia aliahidi kuyafanyia kazi.
“Sisi viongozi wa dini zote kwa uwakilishi tuliomba kuja kukuona mwanzoni kabisa mwa jambo hili na ulitupokea, ukatusikiliza maoni yetu na ukaahidi maoni hayo utawapa wataalamu wayafanyie kazi kwa uzito unaostahili kwa maslahi mapana ya Taifa,” amesema Dk. Shoo.
Aidha, Rais Samia ametumia maadhimisho hayo kusisitiza kukabiliana na mabadiliko ya tabia ya nchi na kuyatumia kama fursa kupitia kilimo cha umwagiliaji ili kuzalisha mazao kwa wingi yatakayosaidia kuimarisha usalama wa chakula.
Latest
