Rais Samia amteua Mobhare Matinyi kuwa Msemaji Mkuu wa Serikali
- Anachukua nafasi ya Gerson Msigwa iliyokuwa wazi kwa siku nane.
- Alikuwa Mkuu wa Wilaya ya Temeke kwa muda wa siku 91.
Dar es Salaam. Baada ya kutokuwa na msemaji mkuu wa Serikali kwa takriban siku nane, hatimaye, Rais Samia Suluhu Hassan amemteua Mobhare Matinyi kuwa Mkurugenzi wa Idara ya Habari – Maelezo ambaye pia atakuwa msemaji mkuu wa Serikali.
Taarifa iliyotolewa na Ikulu usiku wa leo Oktoba 2, 2023 imebainisha kuwa uteuzi huo unaanza mara moja.
Mobhare Matinyi ni mwanahabari mkongwe na mahiri. Aliwahi kuwa Mhariri wa gazeti la Majira, amekuwa akifundisha diplomasia na mtaalamu wa mawasiliano kwa umma.
Matinyi ambaye alikuwa Mkuu wa Wilaya ya Temeke jijini Dar es Salaam anaenda kujaza nafasi iliyoachwa wazi na Gerson Msigwa ambaye Septemba 23, 2023 aliteuliwa na Rais Samia kuwa Katibu Mkuu Wizara ya Utamaduni, Sanaa na Michezo akichukua nafasi ya Said Othman Yakubu ambaye aliteuliwa kuwa balozi.
Uteuzi wa Matinyi unazima minong’ono ya chini kwa chini iliyokuwa ikiwahusisha baadhi wa waandishi wa habari wakongwe nchini Tanzania kushika nafasi hiyo.
Soma zaidi : Rais Samia apangua vigogo TTCL, Tanesco, vilio vya umeme vikiendelea Tanzania
Matinyi amekuwa Mkuu wa Wilaya ya Temeke kwa muda wa siku 91 pekee ambapo aliteuliwa Julai 2, 2023 akichukua nafasi ya Mwanahamisi Nkunda ambaye uteuzi wake ulitenguliwa.
Uteuzi huo unafanya mpaka sasa kuwe na nafasi mbili za ukuu wa wilaya zilizoachwa wazi ikiwemo ya aliyekuwa Mkuu wa Wilaya ya Korogwe Jokate Mwegelo ambaye jana Octoba Mosi, 2023 Chama Cha Mapinduzi (CCM) kilimteua kuwa Katibu Mkuu wa Umoja wa Wanawake wa chama hicho (UWT).
Latest
