Polisi yakamata watuhumiwa wanne ubakaji wa binti Tanzania
- Watuhumiwa wanne wamekamatwa mikoa ya Dodoma na Pwani
- Uhalifu huo ulitendwa Dodoma wakati mwathirika akitokea Dar es Salaam
Dar es Salaam. Jeshi la Polisi limewakamata watuhumiwa wanne kati ya sita waliohusika katika tukio la ukatili wa kijinsia kwa binti mdogo, siku tano baada ya kusambaa kwa video zilizoleta shinikizo kubwa kwa vyombo vya usalama kutoka kwa wananchi na wanaharakati kuwachukulia hatua wahusika.
Mwishoni mwa juma lililopita vilisambaa vipande vya video zikiwaonyesha wanaume watano wakimfanyia vitendo vya ukatili binti aliyedai kuwa ni mkazi wa Yombo Dovya Shuleni jijini Dar es Salaam wakidai kuwa “wametumwa na afande”.
Kusambaa kwa video hizo kuliibua makundi mbalimbali katika jamii wakiwemo wanasheria, wanaharakati na watumiaji wa mitandao ya kijamii wakitaka polisi wafanye uchunguzi kwa haraka na kuwatia mbaroni wahusika upesi iwezekanavyo ili kuhakikisha binti huyo anapata haki stahiki.
Kwa siku tano, polisi wamekuwa wakieleza kuwa bado wanaendelea na uchunguzi wa tukio na leo Agosti 9, 2024 taarifa iliyotolewa na jeshi hilo imeeleza kuwa imeshawakamata watuhumiwa wanne kati ya sita wa tukio hilo linalohusisha tuhuma za ubakaji na ulawiti.
Watuhumiwa hao, kwa mujibu wa polisi, walikamatwa katika mikoa ya Pwani na Dodoma.
Waliokamatwa na polisi kwa tuhuma hizo ni Clinton Honest Damas maarufu kama Nyundo, Praygod Edwin Mushi, Amini Lord Lema na Nickson Idala Jackson.
“Uchunguzi unaendelea kukamilishwa sambamba na kuwasaka watuhumiwa wawili ambao bado wamejificha ili wafikishwe mahakamani. Kwa hawa ambao bado wamejificha kama kuna yeyote anayefahamu wamejificha kwake atoe taarifa na asipofanya hivyo wakikamatwa wakiwa nyumbani au kwenye makazi yake atakamatwa na kufikishwa mahakamani.” amesema David Misime, Msemaji wa Jeshi la Polisi.
Misime amesema kuwa binti aliyefanyiwa vitendo hivyo ameshapatikana na yupo chini ya uangalizi maalumu akiendelea kupata msaada wa huduma ambazo hufanyiwa mwathirika wa ubakwaji na ulawiti.
Uchunguzi uliofanywa na polisi umebaini kuwa tukio hilo lilitendeka miezi mitatu iliyopita yaani, Mei 2024 eneo la Swaswa mkoani Dodoma.
Aidha Polisi wamewakamata watuhumiwa wengine nane kuhusiana na tukio hilo, wanne ambao ni Frora Mlombola, Agatha Mchome, Madatha Jeremia Budodi na James Nyanda Paul jijini Dar es Salaam kwa kosa la kusambaza video hizo kwenye mitandao ya kijamii.
Wanne wengine ambao ni Amos Lwiza, Adam Dongo, Venance Mallya na Isack Elias kwa kosa la kutengeneza na kusambaza taarifa za uongo zilizosema kuwa binti aliyefanyiwa ukatili amefariki wamekamatwa Arusha na Dar es Salaam.