Mutafungwa: Msifumbie macho wanaovunja Sheria za Usalama Barabarani
- Awataja madereva bodaboda na bajaji kuwa ndio vinara wa uvunjifu wa sheria hizo
- Ndio chanzo kikubwa cha ajali na vifo mkoani Mwanza
Mwanza. Kamanda wa Polisi Mkoa wa Mwanza, Wilbroad Mtafungwa amemuagiza Mkuu Kikosi cha Usalama Barabarani mkoani humo Sunday Ibrahimu kutofumbia macho vitendo vya uvujifu wa sheria vinavyofanywa na madereva wa pikipiki (bodaboda) pamoja na bajaji.
Mutafungwa aliyekuwa akizungumza kwenye kikao cha wadau wa usafirishaji wa abiria kupitia bodaboda, bajaji na bajaji za mizigo leo Juni 8, 2023 amewaambia washiriki kuwa ajali za barabarani hazitapungua kama wao wenyewe hawatobadilika na kufuata kanuni za usafirishaji.
Kwa mujibu wa Mutafungwa kundi hilo ndio wanaongoza kuvunja sheria za usalama barabarani na kusababisha vifo au majeruhi jambo linaloongeza gharama za maisha bila sababu.
Ajali kubwa 81 zilitokea mkoani Mwanza katika kipindi cha Mwezi Januari hadi Disemba mwaka 2022, ambapo watu 71 walifariki na wengine 96 kujeruhiwa huku vifo 25 na majeruhi 26 wakitokana na ajali za pikipiki.
“Niwaagize Mkuu wa salama barabarani (RTO) na DTO wasiwe na huruma kwa madereva kama hao, makosa kama hayo hatarishi kamata peleka vituoni chukua hatua kwa majibu wa sheria,” amesema Mtafungwa
Miongoni mwa makosa yanayosababisha kundi hilo kuwa na ajali nyingi ni kuendesha kwa mwendo kasi pamoja na kutozingatia kanuni za usalama za uendeshaji wa vyombo vya moto ikiwa ni pamoja na kuvaa kofia ngumu.
ili kupunguza na kudhibiti vitendo vya uhalifu ambavyo bodaboda wamekuwa wakihusishwa navyo, Mutafungwa ameagiza kuwepo na uongozi rasmi katika kila kituo ili kubaini wahalifu pale wanapojiunga au wanapofanya tukio.
Namba za bandia tishio
Kwa upande wake Mwenyekiti wa waendesha bodaboda Mkoa wa Mwanza, Marco Masinde ameomba Serikali kufuatilia na kudhibiti wimbi la matumizi ya namba bandia ili kudhibiti vitendo vya kihalifu.
“Pikipiki inapokaguliwa unakuta namba za kuchora zinatofatiana na kadi na hata inapotekea tatizo ukifuatilia namba unakuta iliyokuwepo imetolewa imeweka ile halisi tunaomba suala hili lifuatiliwe kwa kina,” amesema Masinde
kwa mujibu Lugwisha zaidi ya vijana 2,000 wamejiajiri kupitia kazi ya kusafirisha abiria jambo linalochochea maendeleo kwenye jamii.
Latest