Bodaboda, bajaji kushushiwa adhabu za barabarani Tanzania
- Adhabu hizo zinapendekezwa kushushwa mara tatu kutoka Sh30,000 kwa kosa moja hadi Sh10,000.
Mwanza. Serikali ya Tanzania inapendekeza kupunguza adhabu za usalama wa barabarani kwa makosa ya pikipiki na bajaji mara tatu kutoka Sh30,000 hadi Sh10,000.
Iwapo pendekezo hilo litapitishwa na bunge, litatoa ahueni kwa wamiliki wa vifaa hivyo moto vinavyotumiwa zaidi vijana kama sehemu ya ajira.
Waziri wa Fedha na Mipango Dk Mwigulu Nchemba amesema leo bungeni wakati akiwasilisha makadirio ya mapato na matumizi ya Serikali mwaka 2021/22 kuwa vijana wengi wamejiajiri kwenye sekta ndogo ya kuendesha bajaji na pikipiki zikijulikana kama bodaboda.
Dk Nchemba amesema pamoja na kujishughulisha na kazi hizo, vijana hao hupata usumbufu mkubwa wa kulipa faini kutoka kwenye vipato vyao pale panapotokea uvunjaji wa Sheria ya Usalama Barabarani umefanywa na abiria wao.
Ukosefu wa fedha za kulipa adhabu hizo, umesababisha baadhi yao kushindwa kulipa faini na hivyo kuzitelekeza pikipiki zao kwenye vituo vya polisi.
“Mheshimiwa Rais alielekeza jeshi la Polisi kujikita kwenye kutoa elimu kuhusu usalama barabarani badala ya kuwekeza kwenye makosa na kugeuza faini kuwa chanzo cha mapato,” amesema Dk Nchemba na kuongeza;
“Hivyo basi, napendekeza kupunguza adhabu zinazotolewa chini ya Sheria ya Usalama Barabarani SURA 168 kwa makosa ya Pikipiki na Bajaji kutoka Sh30,000 za sasa hadi Sh10,000 kwa kosa moja.”
Lengo la hatua hiyo, amesema, ni kuweka adhabu kwa kuzingatia uwezo wa kulipa.
Hata wakati Serikali ikipendekeza nafuu hiyo ya adhabu, Dk Nchemba ameeleza kuwa adhabu za makosa mengine ya vyombo vya moto zinazotolewa kwa mujibu wa Sheria zinaendelea kubaki kama ilivyo sasa.
Latest