Mufti Mkuu: Viongozi wa dini kemeeni mauaji ya kikatili
- Ni yanayohusisha watu waliopo kwenye mahusiano.
- Ataka viongozi wa dini kuingilia kati.
Dar es Salaam. Wakati matukio ya ukatili wa kijinsia ikiwemo mauaji ya wanandoa yakiendelea kuripotiwa, Mufti Mkuu wa Tanzania, Sheikh Abubakari Zuberi amekemea mauaji yanayoendelea nchini huku akiwataka watu kuzingatia mafundisho ya dini zao.
“Dini haitaki kuiua nafsi nyingine…kuua nafsi ni moja kati ya dhambi kubwa ambazo zitaangamiza watu wengi,” amesema Mufti Zuberi katika hafla ya uzinduzi wa Msikiti wa Masjid Jami’ ul Istiqama, uliozinduliwa na Rais Samia Suluhu Hassan, leo Juni10, 2022 Bukoba, mkoani Kagera.
Mufti Zuberi ametoa wito huo kufutia kuripotiwa kwa mauaji yanayoendelea nchini hasa yanayohusu wanandoa kuuana kwa wivu wa mapenzi.
Sambamba na kukemea vitendo vitendo hivyo, Mufti amesema Serikali peke yake haiwezi kumaliza suala hili la mauaji yanayoendelea kama taasisi za kidini zIsipoingilia kati.
“Nyinyi kama Serikali kulisema likaisha hamuwezi lakini watu wa dini wanaweza kusema na watu wakasikiliza,” amesema Mufti Zuberi.
Soma zaidi:
Katika hafla hiyo, Rais Samia amesisitiza masuala mbalimbali ikiwemo umuhimu wa chanjo ya Uviko-19, Sensa ya Watu na Makazi inayotarajiwa kufanyika Agosti 23 nchi nzima, akiwasisitiza viongozi wa dini zote kwenda kuhimiza suala la sensa kwa waumini wao.
“Sensa hata kwenye dini tunaitumia ili kujipanga vizuri na mambo yetu niwaombe sana Mashekh na viongozi muwahimize wananchi wakashiriki kikamilifu,” amesema Rais.
Rais Samia amehitimisha ziara yake ya kikazi ya siku tatu iliyoanza tangu Juni 8 mwaka huu ambapo akiwa mkoani humo alitembelea kiwanda cha Kagera Sukari na kuweka jiwe la msingi katika awamu ya tatu ya ujenzi wa kiwanda hicho.
Pia alizindua mradi wa maji wa Kyaka Bunazi uliopo Wilaya ya Misenyi pamoja na kuzungumza na wananchi katika uwanja wa Kaitaba.
Latest