Msukumo mpya: Vyuo vikuu vyajinoa kufundisha masomo usafiri wa anga
- Chuo Kikuu cha Mtakatifu Augustine (Saut) kuanza kufundisha somo hilo.
- Itasaidia kuongeza marubani wazawa.
- Pia kuongeza mchango wa sekta ya usafiri wa anga katika pato la Taifa.
Mwanza. Huenda sekta ya usafiri wa anga nchini Tanzania ikapata msukumo mpya baada ya taasisi za elimu ya juu kufungua milango zaidi ya kufundisha masomo ya usafiri wa anga wa kiraia kwa vitendo.
Chuo Kikuu cha Mtakatifu Augustine (Saut) jijini Mwanza na Chuo Cha Kikanda Cha Usafiri wa Anga na Biashara (Regional Aviation & Business College) wamesaini makubaliano ya kuwafundisha kwa vitendo wanafunzi wa chuo kuhusiana na usafiri wa anga wa kiraia.
Akizungumza mara baada ya kusaini makubaliano hayo baina ya pande hizo mbili, Makamu Mkuu wa Saut Profesa Costa Mahalu ameeleza kuwa makubaliano hayo ni ya miaka mitano ambayo yanaaza kuanzia Julai 29, 2022 lengo ikiwa ni kuwawezesha wanafunzi kupata ujuzi kwa vitendo .
Profesa Mahalu amesema wameona wapige hatua kwa kushirikiana na wenzao hasa kwenye masuala ya usafiri wa anga wa kiraia ili wanachuo wajifunze kabla hawajaingia kwenye ajira.
“Wanafunzi wanaomaliza degree zao katika fani ya uhandisi au fani mbalimbali katika ushirikiano wao wanaweza kwenda kusomea kwa vitendo fani mbalimbali katika masuala ya anga kwa kukishirikiana na wenzao ambao wameingia nao makubaliano,”amesema Profesa Mahalu.
Soma zaidi:
- Air Tanzania kuajiri wahudumu wa ndege 88 kuimarisha uendeshaji
- Nini kinafuata baada ya Fastjet kusitisha safari zake?
- Airbus yatundika daruga kutengeneza ndege za kifahari za Airbus A380 Superjumbo
Mkurugenzi Mtendaji wa Chuo cha Regional Aviation & Business Captain Phillemon Kisamo, amesema kozi za usafiri wa anga azifahamiki sana nchini hivyo wameona washirikane na chuo hicho kwa kuwa ushirika wao ni nafasi nzuri ya kutoa fursa kwa vijana wa Tanzania kujifunza ili kukuza uchumi wa nchi.
Kisamo amesema wanahitaji kuwafundisha vijana wa Tanzania ili wawe na ujuzi wa kujiajiri na kuajiriwa pamoja na kukuza sekta ya usafiri wa anga, kupata ajira nje ya nchi mara baada ya kuhitimu na kupata vyeti kwa masomo watakayoyafanya.
“Uchumi wa Tanzania unakuwa kwa kasi na sekta ya anga nayo inakuwa na ukanda wa Afrika Mashariki kuna fursa nyingi za kupata ajira na kuanzisha shughuli ni nafasi nzuri ya sisi kuwa na mahusiano na chuo cha Saut ili kuweza kuwezesha vijana wetu wa Tanzania waweze kuwa na nafasi nzuri ya kufanikiwa katika uchumi hasa tukiangazia sekta ya usafiri wa anga,” amesema Kisamo.
Kwa mujibu wa Kisamo wapo watu wachache ambao wanaweza kuendesha shughuli za anga nchini ambapo katika uendeshaji wa ndege kwa maana ya marubani na mafundi wengi wametoka nje ya nchi.
“Hatuwezi kukua kama vijana hawajasomeshwa katika sekta hiyo na kuona fursa ya kuingia ili wawekeze mawazo yao na mbinu zao ili na wao waanzishe vitu ambavyo vinaweza kuleta matokeo makubwa katika sekta ya anga,,” amesema.
Kwa upande wake Naibu Makamu Mkuu wa Chuo Taaluma- Saut Profesa Hossea Rwegoshora amesema fursa hiyo ni kwao kwa sababu uchumi unakua na usafiri wa anga ni kiwanda kinachokuwa kwa kasi nchini.
“Kwa bahati mbaya sana vyuo vikuu vilikuwa vikiambiwa kwamba vinatoa ujuzi elimu kwa wahitimu wetu lakini watu hawaajiriki hivyo sasa tunatafuta muunganiko kati ya vyuo vikuu na viwanda ili wanachokisoma hapa shuleni waweze kuyafanyia mazoezi kwa vitendo katika maeneo hayo na baadaye waweze kufanya kazi katika maeneo yaleyale, “ amesema Prof Rwegoshora.
Tangazo
