Mchele, unga wa mahindi vyachangia kupaa mfumuko wa bei Oktoba

November 11, 2019 11:29 am · Mwandishi
Share
Tweet
Copy Link
  • Kasi ya mfumuko wa bei za bidhaa na huduma nchini imepanda hadi kufikia asilimia 3.6 kwa mwaka ulioishia Oktoba 2019 kutoka asilimia 3.4 iliyorekodiwa Septemba mwaka huu.
  • Mfumuko huo umechangiwa na  kuongezeka kwa bei za baadhi ya vyakula ikiwemo mchele na unga wa mahindi.

Dar es Salaam. Kasi ya mfumuko wa bei za bidhaa na huduma Tanzania imepanda hadi kufikia asilimia 3.6 kwa mwaka ulioishia Oktoba 2019 kutoka asilimia 3.4 iliyorekodiwa Septemba mwaka huu, ikichagizwa zaidi na kuongezeka kwa bei za baadhi ya vyakula ikiwemo mchele na unga wa mahindi.

Mfumuko wa bei wa Taifa hupima kiwango cha kasi ya mabadiliko ya bei za bidhaa na huduma zote zinazotumiwa na kaya binafsi nchini.

Kwa mujibu wa Ofisi ya Taifa ya Takwimu (NBS), hali hiyo inamaanisha kuwa kasi ya mabadiliko ya bei za bidhaa na huduma kwa mwaka ulioishi Oktoba 2019 imeongezeka ikilinganishwa na kasi iliyokuwepo mwaka ulioishia mwezi Septemba mwaka huu. 

“Mfumuko wa bei kwa bidhaa za vyakula na vinywaji baridi kwa mwezi Oktoba umeongezeka hadi asilimia 5.1 kutoka asilimia 4 kwa mwaka ulioishia mwezi Septemba 2019,” inasomeka sehemu ya ripoti ya mfumuko wa bei ya NBS iliyotolewa leo (Novemba 9, 2018).


Zinazohusiana: 


NBS imesema kuwa baadhi ya bidhaa za chakula zilizochangia kupanda kwa kasi ya bei kwa mwezi Oktoba ni pamoja na mchele kwa asilimia 6.1 na unga wa mahindi asilimia 20.5.

Bidhaa nyingine ambazo kasi ya mfumuko wa bei imepanda ni nyama asilimia 2.2, samaki (16.4), unga wa muhogo kwa (10.9), maziwa ya ng’ombe (3.6), mafuta ya kupikia (7), maharagwe(4.9), mihogo mibichi (17) na viazi vitamu kwa asilimia 8.7.

Bidhaa za vyakula hutumika zaidi katika kaya za Tanzania kutokana na umuhimu wake kwenye maisha ya kila siku na pia ni chanzo cha kipato kwa familia  zinazojishughulisha na kilimo cha mazao na uzalishaji viwandani. 

Kupanda kwa kasi ya mfumko wa bei pia kumeshuhudia katika nchi jirani za Afrika Mashariki ikiwemo Uganda na Kenya. 

Nchini Kenya, mfumuko wa bei umeongezeka hadi asilimia 4.9 kwa mwaka ulioishia Oktoba 2019 kutoka asilimia 3.8 iliyorekodiwa mwaka unaoishia Septemba 2019. Kwa Uganda umeongezeka kwa asilimia 2.5 kutoka asilimia 1.9 katika kipindi hicho. 

Follow Us on TikTok

FOLLOW NOW

Subscribe to Our YouTube Channel

SUBSCRIBE NOW