Mbivu, mbichi kesi ya Lissu kujulikana Agosti 18

August 13, 2025 3:06 pm · Kelvin Makwinya
Share
Tweet
Copy Link
  • Ni baada ya Hakimu Mkazi Mkuu wa Mahakama ya Kisutu, Franco Kiswaga kuahirisha shauri hilo hadi tarehe hiyo ili kutoa amri ndogo (orders) kuhusu ombi na pingamizi lililowasilishwa.

Dar es Salaam. Hatma ya urushaji wa moja kwa moja wa mwenendo wa kesi ya uhaini inayomkabili Mwenyekiti wa Chama cha Demokrasia na Maendeleo (Chadema), Tundu Lissu, itajulikana Agosti 18, 2025.

Hii ni baada ya Hakimu Mkazi Mkuu wa Mahakama ya Kisutu, Franco Kiswaga kuahirisha shauri hilo hadi tarehe hiyo ili kutoa amri ndogo (orders) kuhusu ombi na pingamizi lililowasilishwa.

Uamuzi huo umetolewa baada ya upande wa Jamhuri kuomba kesi hiyo isirushwe mubashara kwa lengo la kulinda utambulisho wa mashahidi raia, ukieleza kuwa hata bila kutaja majina, maelezo ya ushahidi yanaweza kufichua utambulisho wao,ombi ambalo limepingwa na upande wa utetezi.

Kwa mujibu wa Wakili wa Serikali Mkuu Nassoro Katuga msingi wa ombi hilo unatokana na uamuzi wa Mahakama Kuu wa Agosti 4, 2025, ulioelekeza mashahidi raia kulindwa kwa kutoa ushahidi kwa kificho na taarifa zao kutochapishwa bila idhini ya Mahakama.

Hata hivyo, Lissu amepinga vikali ombi hilo, akisisitiza kuwa Mahakama Kuu haijaamua kuhusu urushaji mubashara ambapo amesema kupiga marufuku matangazo ya mubashara ya  televisheni kutarejesha mfumo wa zamani wa mahakama za ndani “star chamber court” uliokandamiza haki. 

“Hakuna hoja hapa ya kwamba televisheni zizimwe,” amesema Lissu.

Mara baada ya mabishano ya hoja za pande zote mbili Hakimu Franco Kiswaga amesema uamuzi wa Mahakama Kuu kuhusu ulinzi wa mashahidi unawahusu mashahidi raia pekee, si wote. 

Kiswaga ameongeza kuwa msimamo wa mahakama utatolewa Agosti 18, siku ambayo kesi pia itaendelea kwa hatua ya kuipeleka Mahakama Kuu kwa usikilizaji wa ushahidi.

Lissu, ambaye anakabiliwa na mashtaka ya uhaini, alikamatwa Aprili 9,2025, akiwa katika mkutano wa Chadema huko Mbinga, mkoani Ruvuma, na kusafirishwa hadi Dar es Salaam, ambapo alifikishwa mahakamani Aprili 10, 2025.

Follow Us on TikTok

FOLLOW NOW

Subscribe to Our YouTube Channel

SUBSCRIBE NOW