Mbeya, Kigoma kupata rada za kuangazia hali ya hewa
- Hatua hiyo inatokana na Mamlaka ya Hali ya Hewa Tanzania (TMA) kusaini mkataba wa ununuzi wa rada mbili za hali ya hewa na kuifanya Tanzania kuwa na mtandao wa rada tano.
- TMA tayari imeifunga rada mbili za hali ya hewa huko Kiseke Mwanza na Bangulo Dar es Salaam ambapo imeanza utaratibu wa ufungaji wa rada mkoani Mtwara.
- Rada inasaidia kujua kwa wakati maeneo yenye mvua, aina ya mawingu yaliyopo, muelekeo wa mifumo inayosababisha hali mbaya ya hewa ikiwemo vimbunga na upepo mkali.
Dar es Salaam. Mamlaka ya Hali ya Hewa Tanzania (TMA), imesaini mkataba wa ununuzi wa Rada mbili za hali ya hewa zitakazofungwa eneo la Kawetere katika Halmashauri ya Jiji la Mbeya na eneo la Nyamoli katika barabara ya kuelekea Bulombora, Kigoma na hivyo kuifanya Tanzania kuwa na mtandao wa rada tano.
Tukio hilo limefanyika leo (Aprili 1, 2019) ambapo TMA imeingia mkataba huo na kampuni ya Enterprise Electronics Corporation (ECC) ambayo ni mtengenezaji wa rada hizo.
TMA tayari imeifunga rada mbili za hali ya hewa huko Kiseke Mwanza na Bangulo Dar es Salaam ambapo imeanza utaratibu wa ufungaji wa rada nyingine mkoani Mtwara.
Hii inaifanya mamlaka hiyo kuwa taasisi bora kwa uangazi wa hali ya hewa kwa njia ya rada katika ukanda wa Afrika Mashariki na Kati.
Kwa mujibu wa taarifa iliyotolewa na TMA, ununuzi wa rada hizo mbili (ya nne na ya tano) kwa ajili ya Mbeya na Kigoma umegharimu kiasi cha Sh5.7 bilioni (Dola za Marekani 2.49 milioni) kwa kila moja na pia utengenezaji na ufungaji wa rada zote mbili utachukua muda wa miezi 18 hadi kukamilika kwake.
“Rada hizo zina uwezo wa kuona hadi kilometa za mkato 450 (Aerial distance) huku zikizunguka (radius distance) na uwezo halisia wa kuona mpaka matone madogo sana ya mvua ni kilometa za mkato 250,” inasomeka sehemu ya taarifa hiyo.
Rada za hali ya hewa ni moja ya mitambo inayotumika kufanya uangazi wa hali ya hewa wa masafa marefu. Mitambo hiyo husaidia katika kukusanya data za hali ya hewa zinazoonesha uhalisia wa anga kipindi rada inapozunguka.
Soma zaidi:
- TMA yatahadharisha ujio mvua kubwa
- Watanzania washauriwa kutumia taarifa za hali ya hewa kwenye mipango ya maendeleo
- Ujio mfumo wa taifa wa hali ya hewa kuchochea ujenzi wa viwanda nchin
- Usafiri, biashara kuwa sehemu ya mwelekeo hali ya hewa Dar
Rada inasaidia kujua kwa wakati maeneo yenye mvua, aina ya mawingu yaliyopo na wakati mwingine hata kujua ni kiasi gani cha mvua kinachotarajiwa na ufuatilia maeneo yenye mvua kubwa na za mawe zinazoambatana na radi na upepo mkali hivyo kuweza kutoa tahadhari kwa muda muafaka.
Pia kufuatilia muelekeo wa mifumo inayosababisha hali mbaya ya hewa (mvua za mawe, upepo mkali na dhoruba), vimbunga baharini kadri ya upeo wake na hivyo kuweza kutoa tahadhari kutokana na mwenendo wa vimbunga hivyo.
Kufuatilia upepo unaoweza kuleta madhara kwa usalama wa usafiri wa anga (wind shear) na kutoa ushauri kwa watumiaji wa huduma za hali ya hewa ili wachukue tahadhari wakati wa shughuli zao kiuchumi na kijamii. Kazi nyingine ni kusaidia kutoa utabiri wa muda mfupi na wakati wa hali mbaya ya hewa.
“Wito unatolewa kwa wananchi wote kutoa ushirikiano katika kulinda na kutunza mitambo hii ya Rada pamoja na vifaa vyote vya hali ya hewa kwa manufaa ya Taifa letu,” imeeleza taarifa hiyo.