Mapato ya dhahabu iliyouzwa nje ya nchi yaongezeka kwa asilimia 45.5 Tanzania
- Ongezeko hilo la mapato hayo ya dhahabu limechangiwa zaidi na kupaa kwa kiwango cha madini yaliyouzwa nje ya nchi na kuongezeka kwa bei katika soko la dunia.
Dar es Salaam. Mapato ya mauzo ya dhahabu nje ya nchi yameongezeka kwa asilimia 45.5 ndani ya mwaka mmoja yakichagizwa zaidi na kupaa kwa kiwango cha shehena iliyouzwa pamoja na bei katika soko la dunia.
Ripoti mpya ya mapitio ya uchumi ya Januari 2020 (Monthly Economic Review) ya Benki Kuu ya Tanzania (BoT) inabainisha kuwa mapato ya dhahabu iliyouzwa nje ya nchi yaliongezeka hadi Dola za Marekani 2.22 bilioni (Sh5.08 trilioni) mwaka 2019 kutoka Dola za Marekani 1.52 bilioni (Sh3.5 trilioni) mwaka 2018.
“Mauzo ya dhahabu nje ya nchi, ambayo ni asilimia 52.3 ya bidhaa zisizokuwa za mazao (non-traditional exports), yaliongezeka kwa asilimia 45.5 hadi Dola za Marekani 2.217 bilioni (Sh5.08 trilioni), yakichagizwa na kuongezeka kwa kiwango na bei katika soko la dunia,” imesema ripoti hiyo ya BoT iliyotolewa mapema wiki hii.
Hata hivyo, benki hiyo haikubainisha kiwango cha shehena ya dhahabu iliyouzwa nje ya nchi mwaka jana.
Serikali ya Rais John Magufuli imekuwa ikifanya jitihada mbalimbali za kuongeza faida za madini Tanzania ikiwemo kubadili sheria na kanuni zinazoziba mianya ya rasilimali hizo kutoweshwa kirahisi nje ya nchi bila kulipa kodi stahiki.
Mapema mwaka jana, Serikali ilianzisha masoko ya madini katika kila mkoa wenye rasilimali hizo ili kuboresha ukusanyaji imara wa taarifa za uzalishaji madini na mapato ya Serikali.
Katika ripoti hiyo, BoT imesema mapato ya jumla ya uuzaji wa bidhaa na huduma nje ya nchi yaliongezeka hadi Dola za Marekani 9.71 bilioni (Sh22.24 trilioni) mwaka 2019 kutoka Dola za Marekani 8.39 bilioni (Sh19.22 trilioni) mwaka juzi.
“Katika miezi ya hivi karibuni, hali iliimarika zaidi kutokana na kuongezeka kwa mapato yatokanayo na huduma na thamani ya bidhaa zisizo za mazao,” imesema BoT.
Dhahabu ni moja ya vyanzo vikubwa vya fedha za kigeni nchini Tanzania sanjari na utalii. Picha|Wikiendi.
Latest
