Mambo muhimu ya kuzingatia kabla, baada ya kununua kondomu
- Ni pamoja na kujua tarehe ya mwisho wa matumizi.
- Pia mazingira huru yanayoruhusu faragha yako.
- Unashauriwa kununua katika duka la dawa au kituo cha afya ili kupata ushauri wa kitaalamu.
Dar es Salaam. Manunuzi ya kondomu huambatana na mambo mengi ikiwemo aibu ya kununua kwa baadhi na wapo ambao hushindwa kabisa kununua bidhaa hiyo na kuondoka madukani baada ya kukutana na watoa huduma ambao wanawaonea aibu.
Jambo hilo huwaweka baadhi ya vijana katika hatari ya kupata maambukizi ya magonjwa yanayoambukiza kwa kujamiiana bila kinga ikiwemo Ukimwi na mengineyo.
Ili kujikinga na magonjwa ambayo yanaambukiza kwa kujamiiana, wataalamu wa afya wanashauri wenza kutumia kondomu na njia zingine za uzazi wa mpango baada ya kuonana na mtaalamu wa afya.
Endapo wenza wataamua kutumia kondomu, yapo mambo ya kuzingatia kabla, baada na wakati wa kununua bidhaa hiyo.
Mraghibishi wa afya ya jamii na njia za kujikinga na magonjwa, Dk Lilian Mwakyosi ameiambia Nukta Habari (www.nukta.co.tz) kuwa, moja ya mambo muhimu ya kuzingatia unaponunua kondomu ni uhuru wako pamoja na faragha.
Mtaalamu huyo amesema, pale mtu anaponunua kondomu katika mazingira ambayo ana uhuru na faragha yake ipo salama, atapata muda wa kusoma maelezo ya kondomu na kufahamu kama inaendana naye.
“Siyo kwamba kununua kondomu madukani ni mbaya, lakini pale unapoenda dukani kwa Mangi kununua kondomu, huenda usipate muda wa kusoma kondomu hiyo kujua kama inakufaa au laa,” amesema Dk Mwakyosi akitofautisha hali hiyo na kununua kondomu katika maduka yanayokuruhusu kujihudumia mwenyewe.
Yapo mengi ya kuzingatia. Kujua zaidi, tazama video hii fupi.
Latest