Mambo ambayo hayatakiwi kufanywa sikukuu ya Eid el-Adha
- Viongozi wa dini waonya matendo haramu wakati wa kusheherekea.
- Kitaifa kuadhimishwa Jijini Dar es Salaam.
- Waislamu watakiwa kuswali sala ya asubuhi na kuchinja wanyama.
Dar es Salaam. Sikukuu ya Eid el-Adha ni moja kati ya sikukuu kubwa zaidi miongoni mwa waumini wa dini ya Kiislamu inayoambatana na shamra shamra nyingi zikiwahusisha pia vijana.
Katika mataifa mengi duniani siku hii huwa ni mapumziko inayowaruhusu waumini wa dini hiyo kupata muda wa kumuadubu Mungu kwa swala kish kujumuika na familia kwa ajili ya kusherehekea.
Kwa mujibu wa tovuti ya Islamic Finder sikukuu hii ni ukumbusho wa dhabihu ambayo Nabii Ibrahim (A.S.) aliitoa kutokana na imani yake thabiti kwa Mwenyezi Mungu.
“Ibrahim (AS) alionyesha nia ya kumtoa kafara mwanawe Nabii Ismail (A.S.) lakini mbadala wake alipewa mwanakondoo na Mwenyezi Mungu.
Mwenyezi Mungu alifurahishwa sana na kujitoa kwa Ibrahim (A.S.) kiasi kwamba utoaji wa dhabihu na imani umekuwa sehemu ya kudumu ya maisha ya Muislamu. Tukio hili limetajwa katika Quran – Surah As-Saffat (37:102),” inaeleza tovuti hiyo.
Nchini Tanzania Baraza Kuu la Waislamu wa Tanzania (Bakwata) lilitangaza hivi karibuni kuwa sikukuu hiyo itasherehekewa Juni 29, 2023 na kitaifa itafanyika mkoani Dar es Salaam.
Zinazohusiana
Hii si siku ya starehe, kujimwaga
Hata wakati Waislamu wakisheherekea sikukuu hiyo si watu wote hususan vijana wanafahamu masuala muhimu ya kuzingatia katika siku hiyo.
Badhi ya viongozi wa dini wameiambia Nukta Habari kuwa siku hiyo haihusishi kabisa masuala ya kupiga muziki au kufanya starehe.
“Watu wanafikiri siku hiyo ni ya uhuru sana, wanapiga miziki, wanakunywa pombe jambo ambalo ni haramu katika dini ya Kiislamu…watu wazingatie kutokufanya matendo hayo,” amesema Sheikh Haidali Maulid wa Msikiti wa Malimbe jijini Mwanza.
Shereherekea kwa kuswali sala ya asubuhi
Kwa waumini wa dini ya kiislamu kuswali sala ya asubuhi siku ya sikukuu ni moja kati ya sun’na zinazotajwa katika vitabu vitakatifu vya dini hiyo hususan ikifanyika wakati wa asubuhi.
“Swala ya Eid huanza kutoka wakati jua linapofikia mita tatu juu ya upeo wa macho hadi jua linapofikia meridiani yake. Hata hivyo, ni bora kuswali saa za mapema baada ya kuchomoza jua. (Abu Dawuud: 1135), imesema tovuti ya Islamic Finder.
Sambamba na hilo katika siku hii waislamu wanashauriwa kutokula chochote wakati wa kwenda kuswali na kufuturu mara baada ya kumaliza swala.

Wanyama wanaochinjwa katika sikuu ya Eid el-Adha ni pamoja na kondooo, ng’ombe, mbuzi pamoja na ngamia.Picha|Global Times.
Chinja wanyama na gawa kwa wahitaji
Sheikh Maulid anasema msingi wa sikukuu hii ni kuchinja wanyama, hivyo baada ya swala namna nyingine ya kusherekea ni kuchinja wanyama, kugawa kwa wahitaji na kula pamoja na familia.
“Muislamu unaruhusiwa kuwaalika watu wote na hata wasio Waislamu…kama ukichinja ng’ombe, mbuzi au kondoo kuna kiwango unatakiwa kuwapa maskini na wasiojiweza,” amesema.
Nayo tovuti ya Islamic Finder imesema nyama inayochinjwa katika siku hii igawanywe mara tatu, robo tatu ya kwanza ni kwa ajili ya familia, ya pili kwa ajili ya wasiojiweza na robo tatu iliyobakia kwa ajili ya wageni na majirani.
Ikiwa Muilsamu hana uwezo wa kuchinja anaweza kununua nyama buchani na kupika na familia au kugawa kwa wahitaji.
Shereherekea kwa staha pamoja na familia, uwapendao
Sikukuu ya Eid al- Adha huambatana na mikusanyiko ya ndugu, jamaa na marafiki kwa ajili ya kupata chakula na kufurahia, Sheikh Maulid anasema mikusanyiko hii ya siku ya eid ni vyema ikifanyike kwa kuepuka kufanya mambo haramu yasiyokubalika.
“Mikusanyiko ya wanawake na wanaume katika siku hii inaruhusiwa ila kila jinsia wakae sehemu yao kisha kama watacheza au kufurahi basi wasihusishe muziki au mambo mengine haramu,” amesema Sheikh Maulid.