Makonda: Hali ya Corona Dar inaendelea kuwa nzuri

May 13, 2020 4:10 pm · Nuzulack Dausen
Share
Tweet
Copy Link
  • Amesema ni moja ya matokeo ya watu kufuata maelekezo ya wataalamu wa afya ya kujikinga na janga hilo.
  • Amesema kuwa ameamua kueleza hali ya ugonjwa huo ili kuondoa fursa kwa watu waovu kutoa taarifa za uzushi mtandaoni.

Dar es Salaam. Mkuu Mkoa wa Dar es Salaam Paul Makonda amesema hali ya maambukizi ya ugonjwa wa virusi vya corona (COVID-19) jijini humo inaendelea “kuwa nzuri” ikiwa ni moja ya matokeo ya watu kufuata maelekezo ya wataalamu wa afya ya kujikinga na janga hilo.

Kiongozi huyo wa juu wa mkoa amewaambia wanahabari leo wakati akipokea msaada wa gari la kupambana na COVID-19 kutoka kampuni ya Tata kuwa taarifa alizonazo kutoka kwa mganga mkuu wa mkoa (RMO) ni kuwa “hali inaendelea kuwa nzuri”.

“Hali siyo mbaya kama ilivyokuwa mwanzo. Hata ile idadi ya watu wanaopiga simu wamechanganyikiwa, wamepanic (wana hofu) imepungua, wagonjwa wanaokuja hospitali ambao wamezidiwa, wana hali mbaya imepungua, tafsiri yake ni nini? Mungu anaendelea kutupa rehema zake, kutulinda na nina uhakika Mungu atatuvusha salama,” amesema Makonda.


Zinazohusiana


Amesema kuwa ameamua kueleza hali ya ugonjwa huo ili kuondoa fursa kwa watu waovu kutoa taarifa za uzushi mtandaoni huku akidai baadhi ya watu wanatengeneza video za mazishi usiku ili kuonyesha hali ni mbaya.

“Wengine wakitengeneza clip (vipande vya video) za uongo, kuna clip moja ilienea nikaamua kufanya kazi ya kufuatilia kumbe watu wamenunua majeneza wameenda kwenye makaburi sehemu wakajaribu kuchimbachimba halafu wakarekodi clip kuonyesha kwamba watu wanazikwa usiku ‘hali ni mbaya mpaka watu wanazikwa usiku’, hapana huu ni uongo na uzushi usioweza kuvumulika,” amesema Makonda.

“Unajiuliza Mtanzania anayefanya hivi inamsaidia kitu gani,” ameongeza bila kueleza maeneo ambayo watu hao walienda kutengeneza video.

Pamoja na kwamba hali inazidi kuwa nzuri, Makonda amesema wakazi wa jiji hilo waendelee kufuata maelekezo ya wataalamu wa afya ikiwemo kuvaa barakoa na kufanya mazoezi.

Kwa mujibu Kituo cha Kudhibiti Magonjwa Afrika (AfricaCDC) hadi sasa Tanzania imerekodi visa 480 vya COVID-19 na vifo 21 huku wagonjwa 167 wakipona ugonjwa huo tangu mgonjwa wa kwanza alivyogundulika katikati ya Machi 2020. 

Follow Us on TikTok

FOLLOW NOW

Subscribe to Our YouTube Channel

SUBSCRIBE NOW