Majaliwa: Wachunguzeni wanaodaiwa kuchoma nyaraka za chuo Sumbawanga

December 16, 2022 7:36 am · Mwandishi
Share
Tweet
Copy Link
  • Mhasibu wa Chuo cha Ualimu Sumbawanga, Eric Rutyamirwa na Mkufunzi wa chuo hicho Godfrey Msenuka.
  • Wanadaiwa kuchoma nyaraka hizo ili kupoteza taarifa za mradi wa ujenzi wa chuo hicho. 
  • Ujenzi wa mradi huo unaojengwa kwa awamu mbili unatarajiwa kugharimu Sh7.1 bilioni.

Dar es Salaam. Waziri Mkuu Kassim Majaliwa amewakabidhi kwa Mkuu wa Taasisi ya Kuzuia na Kupambana na Rushwa (TAKUKURU), Mhasibu wa Chuo cha Ualimu Sumbawanga, Eric Rutyamirwa na Mkufunzi wa chuo hicho Godfrey Msenuka kwa tuhuma za kuchoma moto nyaraka za Serikali na hivyo kupoteza taarifa za mradi wa ujenzi wa chuo hicho. 

Rutyamirwa na Msenuka ambaye alikuwa katibu wa ujenzi  wanadaiwa kuchoma nyaraka hizo na hivyo kupoteza kumbukumbu za ujenzi wa mradi huo ambao manunuzi ya vifaa vya ujenzi yanadaiwa kufanywa mara tatu zaidi ya gharama halisi.

Majaliwa amewakabidhi watendaji hao kwa TAKUKURU jana Desemba 15, 2022 baada ya kukagua maendeleo ya ujenzi wa mradi huo unaojengwa katika kijiji cha Pito Sumbawanga mkoani Rukwa.

Ujenzi wa mradi huo unaojengwa kwa awamu mbili unatarajiwa kugharimu Sh7.1 bilioni na tayari Serikali imeshatoa Sh3.8 bilioni kwa ajili ya awamu ya kwanza. Mradi huo ulianza Agosti 2021 na unatarajiwa kukamilika Januari 2023.

Waziri Mkuu amesema baada ya kubaini kuwepo kwa matumizi mabaya ya fedha za mradi huo na wizara husika kupanga kwenda kufanya uchunguzi ofisi ya mhasibu ambayo ndiyo ilikuwa  na nyaraka iliungua.

 “Nyaraka ziliungua ndani ya ofisi ya Mhasibu huku chanzo cha moto bado hakijajulikana lakini mfumo wa umeme haukuwa na hitilafu ulikuwa salama hata baada ya tukio la  moto kutokea,” amesema Majaliwa. 

Aidha, Waziri Mkuu amehoji ni kwanini mhasibu wa chuo hicho alijipa kazi ya kutunza nyaraka za ujenzi wa chuo hicho kinyume na taratibu kwa sababu aliyepaswa kuwa na nyaraka hizo ni katibu wa kamati ya ujenzi, hivyo aliagiza wote wachunguzwe.

Naibu Waziri wa Elimu,  Sayansi na Teknolojia, Omar Kipanga ametangaza kuivunja kamati ya ujenzi ili kupisha uchunguzi na kuunda kamati mpya ambayo itasimamia ujenzi hadi pale utakapokamilika.

Katika hatua nyingine, Naibu Waziri Kipanga amesema Rais Dk Samia Suluhu Hassan ameridhia kutoa Sh100 bilioni kwa ajili ya kujenga upya vyuo vitano vya ualimu nchini kikiwemo na cha Sumbawanga, Morogoro, Tabora,  Ngara na Kasulu.

Fedha hizo zitatumika katika ukarabati wa vyuo vingine 30 vya ualimu vilivyopo katika maeneo mbalimbali nchini. Serikali ina jumla ya vyuo vya ualimu 35.

Follow us on TikTok

Nukta Habari

FOLLOW NOW
Subscribe to our channel

Nukta TV

SUBSCRIBE NOW
🔴LIVE: ULEGA AKIWASILISHA HOTUBA YA BAJETI YA WIZARA YA UJENZI BUNGENI

🔴LIVE: ULEGA AKIWASILISHA HOTUBA YA BAJETI YA WIZARA YA UJENZI BUNGENI

Nukta TV

🔴LIVE: HOTUBA YA BAJETI YA WIZARA YA ULINZI NA IKISOMWA BUNGENI

🔴LIVE: HOTUBA YA BAJETI YA WIZARA YA ULINZI NA IKISOMWA BUNGENI

Nukta TV

Fahamu kuhusu Virusi vya ‘Hantavirus’ na nini chanzo chake ?

Fahamu kuhusu Virusi vya ‘Hantavirus’ na nini chanzo chake ?

Nukta TV